Thursday 5 September 2013

Serikali iboreshe sekta ya usafirishaji?


Posted  Jumatano,Septemba4  2013  saa 21:10 Pm
Kwa ufupi
Upande wa barabara nako kuna matatizo yake lukuki, imaelezwa kuwa barabara za Tanzania zina vizuizi vingi kiasi cha kuwakwaza wasafirishaji wa mizigo wa ndani na nje ya nchi.


 Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) imetoa takwimu za hali ya uchumi katika kipindi cha robo ya kwanza ya mwaka huu inayohusisha mwezi Januari na Machi.
Kwa mujibu wa takwimu hizo pato la taifa(GDP) limepanda kwa asilimia 7.5 kiwango ambacho ni kikubwa kuliko viwango vingine vya kipindi kama hicho tangu mwaka 2009.
NBS inasema sekta zote za uzalishaji zimefanya vizuri kiuchumi katika kipindi hicho cha miezi mitatu ya kwanza ya mwaka huu na pato hilo limefikia Sh4.5 trilioni.
Miongoni mwa sekta hizo ni sekta ya uchukuzi na mawasiliano ambayo kasi ya ukuaji wake ilifikia asilimia 22.2. Mkurugenzi wa uchumi wa NBS, Morrice Oyuke anasema huduma ya usafiri wa treni jijini Dar es Salaam, maarufu kama treni ya Mwakyembe imechangia kupanda kwa pato katika sekta ya uchukuzi.
Pamoja na habari hizo kwa sekta hiyo ambayo mbali na reli pia inahusisha anga, barabara na maji upande wa pili wa sarafu kwa sasa umegubikwa na hali ya shaka.
Pamoja na sekta ya reli kufanya vizuri, lakini hivi karibuni mgomo wa wafanyakazi wa Shirika la Reli la Tanzania na Zambia (Tazara), umeleta athari kwani matatizo ya Tazara yamekuwa ya muda mrefu na jitihada zinazochukuliwa hazionekani kutoa tiba ya kudumu.
Matatizo haya yanapoendelea yanazorotesha hali ya uchumi.
Kwa upande wa anga, siku za hivi karibuni Uwanja wa Ndege wa Julius Nyerere (JNIA) umekuwa njia ya kusafirishia dawa za kulevya kiasi cha kutia aibu kwani vitendo hivyo havifanani kabisa na jina lenyewe.
‘Unga’ unapitishwa uwanjani hapo huku wahusika wakiwa ‘wamelala’ mpaka Waziri wa Uchukuzi Dk Harrison Mwakyembe alipoingilia kati na kuanza kusafisha.
Nakumbuka Waziri Mwakyembe alisema katika moja ya mikutano yake kuwa aibu hiyo inasababisha Watanzania wasiaminiwe wanaposafiri kwenda mataifa mengine kwa kuhisiwa watakuwa wamebeba unga. Naunga mkono hatua alizoanza kuchukua dhidi wote wanaohusika na uchafu huo.
Upande wa barabara nako kuna matatizo yake lukuki, imaelezwa kuwa barabara za Tanzania zina vizuizi vingi kiasi cha kuwakwaza wasafirishaji wa mizigo wa ndani na nje ya nchi. Kwa mfano, kuna mizani nane kutoka Dar es Salaam hadi Rusumo ulipo mpaka kati ya Tanzania na Rwanda.
Si mizani tu bali na vizuizi vingine vingi vya ukaguzi wa magari yanapokuwa safarini, hali hii inasababisha nchi za Uganda na Rwanda kutaka kujitoa kutumia Bandari ya Dar es Salaam kwa sababau ya vizuizi vingi vinavyochelewesha mizigo yao. Madereva wanaofanya safari hizo wanasema kuna wakati wanakaa kwenye foleni kwa saa tatu katika mzani mmoja, mpaka amalize mizani zote atakuwa amepoteza muda kiasi gani?


Bandari ya Dar es Salaam inalalmikiwa kwa ucheleweshaji wa mizigo huku pia ufanisi wake ukiwa mdogo. Utafiti uliofanywa na mtandao unaojihusisha na ukaguzi wa hesabu KMPG na Benki ya Dunia (WB) unaonyesha kwamba mwezi Mei na Juni 2012, meli za kontena zilikuwa zinapanga foleni kwa wastani wa siku 10 zikisubiri gati katika Bandari ya Dar es Salaam, wakati muda wa kusubiri ulikuwa chini ya siku moja katika Bandari ya Mombasa. Msafirishaji gani anaweza kuvumilia hali hii?
Kwa nini tusifanye mambo kisasa? Tunapoteza fursa kwa sababu ya uzembe. Foleni bandarini, foleni barabarani ukienda uwanja wa ndege unakutana na unga yote haya Tanzania. Kwa nini?
0715 221918.

source: Mwananchi