Thursday 19 September 2013

Vitendo vya tindikali Zanzibar ni uhalifu


  MCL


Posted  Jumatano,Septemba18  2013  saa 9:49 AM
Kwa ufupi
Sidhani kama ule usemi wa Zanzibar ni njema atakaye na aje kama kuna mtu atauamini tena. Iweje vyombo vya dola, hasa polisi wanashindwa


Zanzibar. Niliwahi kusema huko nyuma kwamba Zanzibar haimalizi mwezi bila kuzuka jambo, siku hizi mambo yazukayo ni ya ajabu na yenye kusikitisha sana katika jamii yetu.
Mambo hayo kama hayatashughulikiwa kwa nguvu zote na hasa kama  vyombo vya dola havitojirekebisha katika utendaji wa kazi, inawezekana wananchi wakapungukiwa imani navyo.
Vitendo vya watu wasiokuwa na hatia kumwagiwa tindikali ni vitendo ambavyo vinaweza kutafsiriwa kama ni ishara ya vyombo hivyo kushindwa kutimiza wajibu wao wa kuwalinda raia.
Hii ni kwa sababu tukio la kumwagiwa tindikali kwa Padri wa Parokia ya Machui, Anselmo Mwang’amba limepangwa na kutekelezwa ikiwa ni mwezi mmoja tangu raia wawili wa Uingereza, Kate Gee na Kirstie Trup walipomwagiwa tindikali, maeneo ya Mji Mkongwe wakati wa Magharibi.
Shambulizi hilo lilifanyika katika eneo la Shangani katika Mji Mkongwe wa Zanzibar. Tukio hili ni mfululizo wa matukio kadhaa ya watu kushambuliwa kwa kumwagiwa tindikali hapa Zanzibar.
Baadhi ya matukio, kwa mfano kumwagiwa tindikali kwa Katibu wa Mufti wa Zanzibar,  Sheikh Fadhil Suleiman Soraga, kumwagiwa tindikali kwa aliyekuwa Mkurugenzi wa Baraza la Manispaa hatujapata kusikia kama kuna watu waliokamatwa na kufikishwa mahakani! Ni jambo la kusikitisha na linalovunja moyo kuona kwamba Zanzibar iliyokuwa ikisifika kwa hali ya amani, utulivu na ukarimu wa watu wake leo imekuwa tishio kwa tindikali.
 
Sidhani kama ule msemo wa Zanzibar njema atakaye aje sijui kama kuna mtu anayeweza kuja katika hali kama hii, hivi ninajiuliza inakuwaje  vyombo vya dola hasa polisi wanashindwa kubaini mtandao wa wanaopanga na kutekeleza mashambulizi ya tindikali?
Haiwezekani sehemu kama hii ya Zanzibar  dola  ishindwe kubaini watu wanaojihusisha na matukio ya kihalifu kama hayo ya kuwamwagia tindikali, mpaka lini matukio haya yataendelea Zanzibar?
Ukimya umegubika matukio ya tindikali, hadi leo licha ya kutoa matamko makali, lakini vyombo hivi havijatuambia sisi wananchi vimefikia wapi katika kuwasaka wahalifu.
Sasa, suala la kujiuliza kwa nini matukio haya yanafanyika katika maeneo ya Mkoa wa Mjini Magharibi na si katika mikoa mingine ya Zanzibar?
Pengine, vyombo hivi  vingekuwa na hatua zaidi ya kutafiti kwanini matukio haya yamejikita kieneo? tatizo la kijamii, tatizo la kisiasa, tatizo la uchumi au ni jambo gani hili?
Juhudi za makusudi zichukuliwe katika kukomesha vitendo hivyo na wala suala la siasa lisipewe nafasi katika kuwashughulikia wahalifu hao wanaotaka kuchafua jina zuri la Zanzibar, wanaotaka kuharibu uchumi wa nchi, maana hali hiyo inaweza kuwatisha watalii kutotembelea hapa Zanziba.


Tukiwa raia wema tuungane kwa nguvu moja na Serikali yetu katika kuwatafuta na kuwafichua wale wote wanaohusika na kuwashambuliwa watu kwa tindikali.
Tayari, SMZ kupitia kwa Rais wake na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohammed Shein imetoa msimamo wake katika kuchukua hatua sahihi kukomesha.
Katika maelezo yake, Dk Shein ameliagiza Jeshi la Polisi kufanya uchunguzi wa kina na kukabiliana na matukio yakumwagia watu tindikali.
“Hatuwezi kuviacha vitendo hivi viendelee,ni lazima Polisi wajitahidi kuwasaka na kuwafikisha katika vyombo vya sheria wale wote wanaohusika na vitendo hivyo, lazima sheria ichukue mkondo wake,” aliagiza Dk. Shein.
Je, ni kwa kiasi gani polisi wanaweza kuyafanyia kazi maagizo haya ya SMZ maana huko nyuma yameshatolewa maagizo ya aina hiyo na viongozi mbalimbali kwa nyakati tofauti.
Agizo la hivi karibuni ni la Waziri wa Habari, Utamaduni Utalii na Michezo Zanzibar, Said Ali Mbarouk ameshatoa kauli ya kuwaomba wananchi washirikiane na vyombo vya dola kuwafichua wahalifu waliotenda tukio la kumwagiwa tindikali raia wa wawili wa Uingereza.
“Katika kuhakikisha jambo hilo halipewi nafasi kuendelea tena, Serikali imekusudia kuchukua hatua kadhaa ikiwemo kuendesha uchunguzi mkali wa kuwasaka wahusika ili kuweza kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria,”alisema Waziri Mbarouk.
Tunafarijika kuona kwamba serikali imeahidi sio tu kukomesha vitendo hivyo, lakini pia kuanza kuratibu na kusimamia kwa makini zaidi biashara ya tindikali kwa kutunga sheria itakayoweka masharti maalum.
“Kwa vile bidhaa ya tindikali katika siku za hivi karibuni imeanza kutumika vibaya, SMZ inachukua kila hatua kudhibiti matumizi ya bidhaa hiyo kwa kudhibiti uingizaji, usambazaji, upatikanaji na utumiaji wa tindikali na inazitaka taasisi zote zinazohusika zitimize wajibu wake katika matumizi ya tindikali kwa kutumia sheria iliyopo na kwa haraka kutunga kanuni za kuthibiti uuzaji na matumizi ya tindikali,” alisema Waziri Mbarouk.
Matukio haya yanaacha maswali mengi vichwani mwa watu, lakini ni muhimu  kutoingiza hisia zozote zaidi ya uhalifu maana siyo dini wala siasa inayoeleza mtu au kikundi cha watu kufanya vitendo vya kuvunja sheria kama kilichofanywa. Zanzibar ni moja kati ya nchi zenye historia kongwe ya uvumilivu wa kidini ambapo pia ina historia ndefu ya dini Uislamu na Ukristo.  Hivyo, ni suala lililo wazi kuwa vitendo vya watu kumwagiwa tindikali ni vya kihalifu na hakuna budi tuvikatae.

SOURCE: MWANANHI