Wednesday 4 September 2013

Waliosoma Weruweru watamba kutoa rais wa kwanza nchini


Na Beatrice Moses  (email the author)

Posted  Jumanne,Septemba3  2013  saa 20:41 PM
Kwa ufupi
Weruweru ilijizolea umaarufu kutokana na kutoa elimu bora kwa wasichana ambao wameweza kuendelea hadi kufikia kuwa viongozi, kama Dk Asharose Migiro ambaye alikuwa ni mwanamke wa kwanza kuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa.


Dar es Salaam. Waliosoma katika Shule ya Sekondari ya Weruweru wametamba kuwa wanaamini rais wa kwanza mwanamke nchini anaweza kutoka miongoni wao, kutokana na kiwango cha elimu bora inayotolewa katika shule hiyo.
Hayo ameyabainisha jana Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Umoja wa Wanafunzi waliosoma katika sekondani hiyo, Balozi Mwanaidi Maajar akijibu maswali ya waandishi alipokuwa akizungumzia kuhusu Maadhimisho ya Miaka 50 ya Sekondari ya Weruweru ambapo Waziri Mkuu, Mizengo Pinda anatarajiwa kuwa mgeni rasmi.
“Weruweru ilijizolea umaarufu kutokana na kutoa elimu bora kwa wasichana ambao wameweza kuendelea hadi kufikia kuwa viongozi, kama Dk Asharose Migiro ambaye alikuwa ni mwanamke wa kwanza kuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, tunaamini itakuwa ya kwanza pia kutoa rais mwanamke kwa sababu elimu tuliyoipata inatupa nafasi ya kuweza kufanya lolote,” alisema.
Alifafanua kuwa kuna wanawake wengine waliosoma kwenye sekondari hiyo ambao ni viongozi katika nyanja za wafanyabiashara,madaktari, wanasiasa wanadiplomasia, waandishi, walimu, wahadhiri na wajasiliamali. Alisema wanalenga kukusanya Sh500 milioni katika maadhimisho hayo ya miaka 50.

source: Mwananchi