Wednesday 4 September 2013

Tuzibe nyufa zote kujenga EAC imara


Posted  Jumanne,Septemba3  2013  saa 21:4 PM
Kwa ufupi
Wazo hilo la Mbunge Peter Mathuki kutoka Kenya aliungwa mkono na wabunge wote kutoka Rwanda na baadhi kutoka Kenya, Uganda na Burundi.


Katika siku za hivi karibuni, kumetokea mambo kadhaa yanayoonekana kama tishio kwa uhai na mustakabali ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, EAC.
Kwanza, ulikuwa ni mikinzano kimawazo kati ya Rais Jakaya Kikwete na Paul Kagame wa Rwanda kuhusu njia ya sahihi ya kukabiliana na makundi ya waasi.
Wakati Kikwete akipendekeza njia ya mazungumzo ya amani kama njia ya kupatikana kwa mwafaka bila madhara makubwa kwa pande zote mbili, Kagame kwa upande wake anaona makundi ya waasi yanastahili kupigwa hadi yatokomezwe.
Kagame amekaririwa akisema kujadiliana na makundi hayo ambayo baadhi yanatuhumiwa kuhusika kwenye tukio la kihistoria ya mauaji ya kimbari nchini mwake ni kuwakosea marehemu waliopoteza maisha.
Kwa msimamo na mtazamo wa Rais Kagame, majadiliano na makundi ya waasi ni sawa na kucheza ngoma juu ya makaburi ya waliokufa kwenye mauaji hayo ya watu zaidi ya 800,000.
Msigano wa kimawazo na mtizamo baina ya Kikwete na Kagame ‘yamehanikizwa’ na kikao cha Kagame na wenzake, Uhuru Kenyatta wa Kenya na Yoweri Mseveni wa Uganda jijini Kampala na kujadili ushirikiano mpya kati ya nchi hizo katika sekta ya usafirishaji, hasa reli na Bandari ya Mombasa.
Wakati vumbi hilo kati ya wakuu hao wawili likiendelea, jambo lingine limeibuka wiki iliyopita wakati wa vikao vya Bunge la Afrika Mashariki, EALA.
Wabunge wake tisa kutoka kila nchi mwanachama waliingia kwenye mvutano mkubwa miongoni mwao baada ya hoja ya kutaka vikao vya Bunge hilo kufanyika kwa kupokezana kutoka nchi moja hadi nyingine.
Wazo hilo la Mbunge Peter Mathuki kutoka Kenya aliungwa mkono na wabunge wote kutoka Rwanda na baadhi kutoka Kenya, Uganda na Burundi.
Mathuki aliwasilisha hoja ambayo ilipata upinzani kutoka kwa wajumbe wengine waliodai haikuzingatia kanuni na taratibu zinazoelekeza hoja zote kuwasilishwa mezani kwa spika na kuwekwa kwenye orodha ya mambo yanayostahili kujadiliwa.
Baada ya hoja yao kupingwa, wabunge wote kutoka Rwanda hawakuhudhuria kikao kilichofuata na hivyo spika wa Bunge hilo, Magreth Zziwa kutoka Uganda kuahirisha kikao hadi siku iliyofuata.
Kama mchezo wa kuigiza, siku ya pili, wabunge kutoka Tanzania, wakiongozwa na Abdulah Mwinyi nao wakawasilisha hoja ya kuelezea kusikitishwa na kitendo cha wenzao kukwamisha kikao na ili kuonyesha ‘hasira’ zao, nao wakatoka nje ya ukumbi wa kikao.

Uamuzi wa wabunge wa Tanzania nao kususia kikao kikasababisha bunge kushindwa kuendelea kwa siku ya pili kutokana na kanuni ya Bunge hilo linaloelekeza vikao kufanyika baada ya kuwepo uwakilishi wa wajumbe kutoka nchi zote tano wanachama ambazo ni Rwanda, Burundi, Uganda, Kenya na Tanzania, kila kimoja kina uwakilishiwa wabunge tisa.
Kila mmoja anaweza kuwa na tafsiri yake kuhusu matukio hayo mawili, kwanza tofauti ya kimtazamo kati ya Kikwete na Kagame kwa upande mmoja na mvutano kati ya wabunge wa EAC.
Kwa upande wangu, matukio haya mawili yana dalili mbaya kwa EAC kwa sababu yametupa picha na fursa ya kuweka kujua nyufa zinazoikabili jumuiya hiyo ili tutafute mbinu ya kuyakabili na kuyaepuka madhara mengine makubwa siku zijazo.
EAC imejengwa upya baada ya ile ya awali iliyohusisha Tanzania, Kenya na Uganda kuvunjika mwaka 1977.
Tunahitaji kuwa na EAC imara isiyoyumbishwa na tofauti ka ya viongozi tunaowapa dhamana ya uongozi. Tunataka tujenge EAC iliyozama na kuota mizizi miongoni mwa wananchi wake watakaosimama kidete kuilinda dhidi ya viongozi wabinafsi wanaoweza kujaribu kulivunja kwa maslahi au utashi wao binafsi.
Nikitumia mfano wa Mwalimu Julius Nyerere (marehemu), EAC ni sawa na nyumba ambayo uimara wake hujulikana pale tufani inapovuma na kutikiswa.
Jumuiya yetu imetikiswa na matukio hayo mawili, Tayari tumeshuhudia penye udhaifu. Sasa turekebishe ili kuepuka madhara zaidi sasa na baadaye.
Nasema matukio haya ni fursa ya kipekee kwetu sote kujua maeneo ya kurekebisha wakati tukiendelea na juhudi za kufikia hatua ya juu ya ushirikiano wa kisiasa, Shirikisho.
Katibu Mkuu wa EAC, Dk Richard Sezibera anasema mivutano hayo haina madhara kwa jumuiya kwa sababu imejengwa katika msingi imara usioyumbishwa na tofauti na mivutano midogo midogo miongoni mwa viongozi au taasisi zinazohusiana na jumuiya.
psaramba@gmail.com, +255 766 434 354.

source; Mwananchi