Watoto wachanga baada ya kuzaliwa katika Manispaa ya Morogoro, ongezeko 
la wazazi kutupa watoto wao limekuwa likiongezeka nchini. Picha ya 
Maktaba. 
            
    Na Dinna Maningo, Mwananchi
Posted Jumatano,Septemba11 2013 saa 15:30 PM
Posted Jumatano,Septemba11 2013 saa 15:30 PM
Kwa ufupi
Mume anapohisi mtoto aliyezaliwa hafanani nae, 
jambo kuu linalofanywa ni kuua mtoto ili kuifanya ndoa iendelee kuwepo 
au la mke atarajie mateso au hata talaka. 
Tarime. Waswahili husema, mapenzi matamu pale yanapokolea, lakini hugeuka shubiri pale yanapochacha.
Ukweli wa mambo hayo unadhihirika katika maeneo 
mbalimbali ya Wilaya ya Tarime mkoani Mara ambako imebainika kuwa idadi 
kubwa ya wanawake, wasichana wanaotoa mimba au kuua watoto wanaowazaa ni
 kwa sababu ya mapenzi au kukubaliana na wenzi wao.
Wengine huwanyonga, kuwatupa vichanga au watoto 
wadogo kwa sababu ya kuchuja mapenzi au kwa sababu wamekubaliana na 
wenza wao wawaue watoto labda kwa sababu hawafanani na mume.
Ukosefu wa uaminifu kwa wapendanao, hususan 
waliomo kwenye ndoa imekuwa ni sababu ya wahusika kukata tamaa, jambo 
ambalo limesababisha watoto wanaozaliwa kufanyiwa ukatili na hata 
kuuawa.
Utafiti uliofanywa katika wilaya hiyo umebaini 
kuwa watoto wengi wanaozaliwa na kutupwa ni wale ambao wazazi wao ama 
wapo kwenye ndoa au uchumba, ambao watu wake hawaelewani.
Kwa upande wa wanawake, yule aliyekuwa na uhusiano
 na mwanamume mwingine na kwa bahati mbaya akapata ujauzito nje ya ndoa 
hujikuta akilazimika kutoa mimba au kutupa mtoto pindi anapojifungua ili
 kunusuru ndoa au uchumba.
Kadhalika, mwanamume anapomuhisi mkewe kuwa 
alikuwa na uhusiano ya kimapenzi na mwanamume  mwingine, ajifunguapo 
mtoto, humshawishi mke au au yeye huwadhuru wote kwa pamoja.
Pia, mama akishajifungua na baba akaona mtoto 
hafanani naye, humshawishi mama kumuua mtoto. Matendo haya jambo 
yanaonekana kupigiwa kelele mno na vyombo vya dola, bado yanaendelea kwa
 siri kubwa katika baadhi ya maeneo.
Ushuhuda na hali halisi
Ipo mifano kadhaa ya matukio kama hayo kwani 
wilayani Musoma mwaka 2011, aliyekuwa Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mara,
 Robert Boazi ambaye kwa sasa yuko Kilimanjaro aliwahi kuwakamata wazazi
 ambao walishirikiana kuua mtoto na kisha kumtupa.
Kisa ni nini ? 
Ni baada ya baba kudai kuwa mtoto yule aliyezaliwa si wake, bali mwanamke alipewa uja uzito na mwanamume mwingine.
Sufiani Mageta, ambaye ni Katibu wa Afya katika Hospitali ya 
Wilaya ya Tarime anasema kuwa wao hupokea watoto wachanga wanaotupwa 
baada ya kuzaliwa, baadhi yao hukutwa wakiwa hai na wengine wakiwa 
tayari wamekufa.
Anasema kwa mwaka jana pekee, watoto watatu hai 
waliokotwa wakiwa wametupwa na sasa wanalelewa katika kituo cha kulelea 
watoto yatima kilichopo mjini Musoma.
Askofu Isaac Kitongo wa Kanisa la Jeshi la Wokovu,
 Divisheni ya Tarime anasema kuzaa mtoto nje ya ndoa husababisha baadhi 
yao kutelekezwa.
 Ofisa Habari wa Halmashauri ya Wilaya ya Tarime, 
Magreth Segu anasema: ”Wanaume wa siku hizi wengi, wao wanakataa kuishi 
na mtoto wa kambo,  hata wakiishi nao wanawanyanyapaa na wengine 
wamefikia hatua ya kuwaua kwani anaona ni aibu kwa rafiki zake kuwa 
ameoa mwanamke mwenye mtoto”.
 Abel Gicheina, Ofisa wa Ustawi wa Jamii katika 
Hospitali ya Wilaya ya Tarime anasema: “Siku hizi wengi wanaonekana 
wanaingia kwenye uhusiano kwa kuwa na tamaa zaidi ya upendo wa kweli”.
Ofisa Ustawi wa Jamii wa Wilaya ya Tarime, Mwasiti
 Itumbo anasema kuwa zaidi ya kesi 20 zimeripotiwa mwaka jana ofisini 
kwake na zote zinazohusu  wanandoa kutoka nje ya ndoa na tatizo la 
wanaume kutokutoa huduma ya matunzo kwa watoto wanaowazaa.
Itumbo anasema kuwa wanaume hudai kuwa hawatoi matunzo kwa watoto wanaozaliwa kwani wanakuwa si damu yao.
Wanawake kwa upande wao, wanajitetea kuwa wanatoka
 nje ya ndoa kutokana na baadhi ya wanaume kutotoa matumizi ya kutosha 
kwa familia zao, badala yake  wengi wao huwajali zaidi wanawake wa nje 
ya ndoa.
Ingawa si wote wenye tabia hii ya kutoka nje ya 
ndoa, jambo hilo, ofisa huyo anasema  ndilo linalowafanya  wanawake nao 
watoke nje ya ndoa  kutafuta watu wa kuwapa mahitaji, baadhi yao 
hujikuta wamepachikwa uja uzito nje ya ndoa.
 Lucy John, mkazi wa Tarime (si jina lake halisi) 
anasema kuwa baadhi ya  wasichana ambao hawajaolewa wakiwamo wanafunzi  
wanasema kuwa wataacha kutoa mimba iwapo wanaume wanaowabebesha mimba 
watakuwa tayari kulea watoto kwani wengi wao wamekuwa wakikataa ujauzito
 na wanaposhtaki polisi hawaoni hatua za kisheria zikichukuliwa dhidi ya
 wanaume.
Kauli ya RPC 
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kipolisi wa 
Tarime/Rorya, Justus Kamugisha anasema kuwa kwa mwaka 2011-2012, zaidi 
ya watoto wanane wachanga walikutwa wametupwa wamekufa na wengine wakiwa
 hai na kuongeza kuwa watuhumiwa watano walifikishwa mahakamani.
Wengine wamehukumiwa kifungo na kesi nyingine zimefutwa kwa kukosekana ushahidi na sababu mojawapo kubwa ni kutokana na jamii kutokusaidia kutoa ushirikiano Polisi wakati wa upelelezi.
Wengine wamehukumiwa kifungo na kesi nyingine zimefutwa kwa kukosekana ushahidi na sababu mojawapo kubwa ni kutokana na jamii kutokusaidia kutoa ushirikiano Polisi wakati wa upelelezi.
 Kamanda Kamugisha anaitaka jamii kushirikiana  na
 polisi kuwafichua wale wanaobeba mimba na kisha kutoa mimba au kuua  
watoto wao ili wachukuliwe hatua zi kisheria.
Anaeleza kuwa jamii ndiyo ipo karibu na wahusika 
wa tukio, wamekuwa hawako wazi kuwafichua waovu, jambo ambalo linawapa 
ugumu polisi wakati wa upelelezi wao, kiasi kwamba wengine huficha 
watuhumiwa.
SOURCE: MWANANCHI
SOURCE: MWANANCHI
