Monday 2 September 2013

Mwanamke mwenye ndoto ya kuwaunganisha wajane nchini



 
Na Elias Msuya  (email the author)

Posted  Jumapili,Septemba1  2013  saa 13:51 PM
Kwa ufupi
Mbali na kufikisha kilio cha wajane, anasema ziara hiyo ina lengo pia kuhamasisha utalii wa ndani kwa kutembelea maeneo ya kihistoria kama hayo yakihusisha shughuli za kiutamaduni.


Japo ujane unachukuliwa kama hali ya ukiwa kutokana na mwanamke kufiwa na mumewe, lakini hali hiyo sasa kwa wanawake imekuwa changamoto nchini katika kujiletea maendeleo.
Grace Mahumbuka ni mjane anayeishi wilayani Karagwe mkoani Kagera, ambaye sasa ameamua kuanzisha kikundi cha wajane akiwa na ndoto ya kuwangusha wajane nchini ili kujiletea maendeleo ya kiuchumi na jamii.
Mwanamke huyo ambaye pia ni mjumbe wa Baraza Kuu la Jumuiya ya Wanawake wa CCM (UWT), ni Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake Wajane katika Wilaya ya Karagwe na Kyerwa (UWK) ulio na jumla ya wanachama 685.
“Kuwa mjane siyo kubweteka, nimeamua kuwaunganisha wanawake wajane ili tujiletee maendeleo. Tangu mume wangu alipofariki nimekuwa na mtazamo wa kuwatafuta wanawake walio kama mimi ili tuungane katika kupambana na umasikini,” anasema Grace na kuongeza:
“Kwa sasa tuna mradi wa ushirika wa kuweka na kukopa (Saccoss) unaotuwezesha kukopa na kufanya miradi ya maendeleo.”
Anafafanua kuwa, mwamko wa kutetea wanawake wajane umeelekezwa pia katika mabadiliko ya Katiba, akieleza kuwa wamepeleka maoni yao kwenye Mabaraza ya Katiba ili yaingizwe kwenye Rasimu ya Katiba.
“Rasimu ya Katiba haitambui wanawake wajane, sana sana inazungumzia haki za wanawake kwa jumla katika ibara ya 46. Tunataka walau kuwe na ibara ya 46 (b) ili kundi hili nalo likumbukwe. Tulipeleka maoni yetu na sasa tunatarajia kuwa yataingizwa kwenye Katiba Mpya,” anasema Grace.
Anaongeza: “Kwa kuwa wajane tunajitegemea wenyewe katika shughuli zetu, Katiba itoe msamaha walau wa kodi kwenye biashara au unafuu kwenye kipato chetu ili tujimudu kimaisha.”
Kuhusu mikakati mingine, Grace anasema kuwa sasa wanapanga ziara ya kumtembelea Mama Maria Nyerere, ambaye pia ni mjane nyumbani kwake Mwitongo Butiama mkoani Mara, ikiwa ni sehemu ya kuhamasisha umoja wa wanawake wajane nchini.
“Juhudi zetu hazitafanikiwa bila kumshirikisha mjane mwenzetu aliye na hadhi kubwa yaani, Mama Maria Nyerere. Yeye anajua uchungu wa kuwa mjane, hivyo atatusaidia kuwahamasisha wanawake wengine na Serikali kwa jumla. Tutatumia ziara hiyo pia kuzuru kaburi la Mwalimu Nyerere na kufikisha kilio cha wajane nchi nzima,” anasema.
Anasema kuwa katika mikakati yao wameushirikisha uongozi wa Wilaya ya Karagwe, Mkoa wa Kagera, Bunge na Serikali Kuu.
“Tunataka ziara hiyo iwe na siku maalumu ya maadhimisho ya kazi za wajane na tumemwomba Waziri Mkuu Mizengo Pinda kuwa mgeni rasmi. Tumewashirikisha pia Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya makazi, Profesa Anna Tibaijuka na Spika Anna Makinda. Hayo yote yako kwenye maandalizi ili kuhakikisha kuwa ziara yetu inafanikiwa kuleta mwamko kwa wanawake wajane nchini,” anasema.
Mbali na kufikisha kilio cha wajane, anasema ziara hiyo ina lengo pia kuhamasisha utalii wa ndani kwa kutembelea maeneo ya kihistoria kama hayo yakihusisha shughuli za kiutamaduni.
Mbali na kutembelea kwa Mwalimu Nyerere, Grace anasema kuwa pia watatembelea Hifadhi ya Taifa ya Serengeti kwa lengo hilo hilo la kuhamasisha utalii wa ndani.
“Tunaandaa vazi la asili za mwanamke wa Tanzania ambalo litaonyeshwa wakati wa ziara hiyo. Huo ni mchango wetu tulioutoa kwenye kamati ya Taifa ya vazi la Taifa. Lengo ni kuwa na vazi la kitaifa siyo kuendeleza mavazi ya tamaduni za wengine,” anasema na kuongeza:
“Tumeishirikisha Mamlaka ya Hifadhi za Taifa (Tanapa) katika kuhamasisha utalii wa ndani, pia kutakuwa na wasichana 20 watakaoshiriki katika maonyesho hayo ya mavazi.”
Kazi nyingine ya sanaa ambayo itafanywa na kikundi hicho wakati za ziara hiyo Butiama ni kuimba nyimbo zilizoko kwenye albamu waliyoiandaa.
“Tunazo nyimbo tisa katika albamu yetu ambazo zitazinduliwa Butiama baadhi zikiwa ni Umoja wa wajane ulipoingia, Kilimo kwanza, Mama na Tanzania nakupenda. Nyimbo hizo ni moja ya kazi zetu katika kikundi,” anasema.
Akizungumzia malengo ya baadaye, Grace anasema kuwa wanakusudia kufungua chuo cha sanaa watakachokitumia kuwafundisha watoto yatina sanaa za mikono na maonyesho.
“Tunaomba Serikali na wadau wengine watuunge mkono ili kufanikisha jitihada za wanawake kujikomboa,” anasema Grace.

source: Mwananhi