Monday 2 September 2013

Pato la taifa laongezeka



Na Zacharia Osanga, Mwananchi  (email the author)

Posted  Agosti31  2013  saa 23:15 PM
Kwa ufupi
Mkurugenzi wa Uchumi katika Ofisi ya Taifa ya Takwimu, sekta zote za kiuchumi zimefanya vizuri isipokuwa ya madini.


Dar es Salaam. Pato la Taifa (GDP)limeongezeka kwa asilimia 7.5 katika kipindi cha robo ya kwanza ya mwaka huu ikilinganishwa na asilimia 7.4 ya kipindi kama hicho mwaka jana.
Taarifa iliyotolewa jana jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi wa Uchumi katika Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) Morrice Oyuke, imesema kuwa katika kipindi hicho sekta zote za uchumi zilifanya vizuri, isipokuwa sekta ya madini iliyoshuka kutokana na bei ya madini katika soko la dunia kushuka.
Oyuke alibainisha kwamba katika kipindi hicho cha miezi mitatu, pato la taifa lilifikia Sh4. 5 trilioni tofauti na Sh4.2 trilioni kwa kipindi kama hicho mwaka uliopita.
Alisema sekta ya uchukuzi na mawasiliano ilikuwa hadi kufikia asilimia 22.2, wakati huduma za usafiri wa treni ya abiria iliyoanzishwa jijini Dar es Salaam mwishoni mwaka jana, ikichangia ongezeko hilo.
“Shughuli za kilimo na uvuvi zilifikia asilimia 1.4 ikilinganishwa na asilimia 0.4 ya kipindi kama hicho mwaka jana,” alisema mkurugenzi huyo.
Alisema shughuli za uzalishaji viwandani zilikuwa hadi kufikia asilimia 8.6 ikilinganishwa na asilimia 5.7 mwaka uliopita.
“Ukuaji katika sekta hiyo ulichangiwa na kuongezeka la uzalishaji wa vinywaji, bidhaa za tumbaku na sukari,” alinena .
Alisema mafuta na gesi vilichangia ongezeko la ukuaji wa nishati ya umeme kwa asilimia 6.3 ikilinganishwa na asilimia 5.1 katika mwaka jana.
Mkurugenzi huyo alisema shughuli za uchimbaji madini, mawe na kokoto zilishuka kwa asilimia 4.7 ikilinganishwa na asilimia 23.8 mwaka uliopita.