Monday 2 September 2013

Ustawi wa kila mtoto ni muhimu kwa taifa(2)



Posted  Jumapili,Septemba1  2013  saa 14:11 PM
Kwa ufupi
Kwa ufupi, ili mtoto aishi na baba na mama yake, lazima kila aliye mzazi atambue kuwa bila mwenzi wake, mtoto asingepatikana, hivyo awe tayari kumwezesha mtoto kuishi karibu, hata kama siyo pamoja na mzazi wake mwingine.


Mada hii ilianza Jumapili iliyopita; Iliishia kutoa amelezo kuhusu haki ya mtoto kuishi na baba na mama, bila kujali wametengana au la.
Kutokana na sababu mbalimbali, wazazi wengi wanaishi sehemu tofauti. Ikiwa utengano huo unatokana na makubaliano yenye lengo la kunufaisha familia husika; mara nyingi huwa hakuna tatizo kwa mtoto.
Matatizo hutokea endapo utengano unatokana na uhusiano ulioleta mtoto au watoto umeshindikana kuendelea. Yaani wazazi kutengana au kuachana.
Iwapo mmoja kati ya wazazi waliotengana hana busara, huruma wala upendo wa dhati kwa watoto husika, huanza kuonyesha ubabe kwa kuzuia upande wa pili kuishi au kuwa karibu na mtoto wake.
Kuzuia huko kunaweza kufanywa kwa maneno, vitendo au kwa mzuiaji kujenga mazingira yasiyo rafiki kwa mwenzi wake kuishi au kuwa karibu na mtoto wake. Jambo hili halikubaliki kwa sababu linamwathiri zaidi mtoto.
Kwa ufupi, ili mtoto aishi na baba na mama yake, lazima kila aliye mzazi atambue kuwa bila mwenzi wake, mtoto asingepatikana, hivyo awe tayari kumwezesha mtoto kuishi karibu, hata kama siyo pamoja na mzazi wake mwingine.
Ili mzazi afanikiwe katika hilo, hana budi kudhibiti tabia za uroho, uchoyo, wizi, uzinzi, ulevi wa kupindukia, kutotekeleza majukumu yake kwa familia, ubaguzi kwa watoto na ubinafsi. Tabia hizi ni kiini cha mtu kushindwa kutekeleza haki za mtoto, hata kama anazifahamu vizuri.
Wajibu wa mtoto kwa wazazi
Kila mtoto analo jukumu la kuheshimu wazazi pamoja na waangalizi wake wote, kama wao wanavyotakiwa kumheshimu.
Kuna wakati mzazi anaweza kutamani kutokuwa na mtoto, kutokana na utukutu wa mtoto wake. Pengine amejitahidi kwa kadiri ya uwezo wake kumfunza mtoto namna ya kuishi vizuri, lakini bahati mbaya mtoto mwenyewe siyo msikivu; watoto lazima watoe ushirikiano kwa wazazi wao.
Jambo hili lipo tangu enzi, ndiyo maana hata wahenga walitoa usemi kwamba; “Samaki mkunje angali mbichi,” au “Ukichelea mwana kulia utalia wewe,” na nyingine nyingi, lengo likiwa kuwaadharisha wazazi kutolegea na kuacha watoto waendelee na tabia zisizokubalika.
Mtoto asiyezingatia heshima, asitegemee kuwa wanaomlea watazingatia baadhi ya haki zake; kwa sababu ili arejeshwe kwenye mstari uliyonyooka, pamoja na mbinu nyingine ni kufinya baadhi ya haki zake.
Mathalani kumzuia kushiriki michezo kwa kipindi fulani, hadi atakapobadili tabia isiyokubalika kwa mujibu wa mazingira na jamii aliyomo.
Kila mtoto anao wajibu wa kusaidia wazazi, walezi, ndugu na jamaa zake wote walio katika uhitaji wa msaada ulio ndani ya uwezo wake. Kwa kutimiza wajibu huu, mtoto husika ataondokana na tabia kadhaa mbaya mathalani uvivu, dharau, kujikweza na kutokuwa na ushirikiano na wengine.
Wajibu wa mtoto kwa jamii
Mtoto ni mwanachama kamili wa kila jamii, hivyo anapotazamwa kijamii wajibu wake unabadilika kwa kuongezeka kutegemeana na umri wake.
Lakini ili atekeleze ipasavyo wajibu wake ni lazima awe ametendewa haki ya kueleweshwa vizuri na kwa ufasaha juu ya masuala yanayoihusu jamii husika, kama vile elimu kuhusu Katiba ya taifa lake.
Kila mtoto anawajibu wa kufahamu na kutii taratibu, kanuni na sheria za nchi yake; kuthamini na kuzingatia utamaduni, mazingira asilia pamoja na kanuni zinazolenga kudhibiti mienendo ya tabia zinazotawala mahali pa kuishi, kazi na shuleni.
Wajibu wa watoto kwa wenzao
Adabu ya mtoto inatakiwa kuonekana siyo tu kwa wakubwa bali hata kwa watoto wenzake. Hatakiwi kutumia kisingizio cha kutetea au kutumia haki zake za kisheria au kikatiba, kudhuru wengine, (mtoto au mtu mzima)
Itaendelea wiki ijayo…

source: Mwananchi