Monday 2 September 2013

mwingine hawezi kunimiliki zaidi ya kaka yangu


Na Herieth Makwetta  (email the author)

Posted  Jumapili,Septemba1  2013  saa 14:12 PM
Kwa ufupi
Licha ya kuwepo katika kundi hilo, msanii huyo amepewa uhuru wa kufanya kazi zake binafsi na hivi sasa ameonyesha kufanya kazi nzuri inayopendwa na wengi, hasa anapokuwa katika majukwaa.


“Ukihitaji kufanya kazi na Meninah au kupata taarifa za ndani za msanii huyu, huna sababu ya kuhangaika, bali mtafute kaka yangu Atick maarufu kwa jina la Tik tik.”
Hiyo ni sehemu ya maelezo ya Meninah na ndiyo msimamo wa staa huyo wa Bongo Star Search 2012, Meninah Abdulkarim Atick anayewika na vibao kama ‘Dream Tonight na Shaghalabaghala’, akiamini kuwa kumilikiwa ndugu yake wa damu kutamfanya aweze kuwa huru na imani ya kipato chake, tofauti na mtu mwingine.
“Meneja wangu ni kaka yangu, sidhani kama ninaweza kumilikiwa na mtu mwingine kwani sina imani. Unajua ndugu yako anaweza kuthamini kile ukipatacho na siyo mtu mwingine kwani hana uchungu na wewe. Kaka yangu amenisaidia sana mpaka hapa nilipofika, yeye ndiye aliyekuwa akinipa mwongozo, hivyo namwamini kunisimamia,” anasema.
Meninah anasema kuwa kufanya kazi na mtu baki kumewasababishia wasanii wengi kushindwa kusonga mbele kimaendeleo, hata mameneja wao kuwapoteza katika soko la muziki mara wasanii wanapodai masilahi yao.
“Ni ngumu kufanya kazi na mtu baki,lawama tu, mtatofautiana mwisho wa siku. Kaka yangu ananipenda na ataweza kunisimamia vizuri. Idadi kubwa ya wasanii wanapotea kutokana na meneja husika, wengi hawawasimamii kama inavyopaswa, ikitokea wakatofautiana ni rahisi kumharibia msanii kazi yake. Ni wachache huachana kwa amani,” anasema Meninah ambaye ni mtoto wa mwisho katika familia ya Abdulkarim Atick.
Licha ya kufanya muziki akiwa mwenyewe, Meninah pia anaunda Kundi la Shosteez akiwa sambamba na Nuru Yogo na Salma Mahin, kundi lililoundwa na prodyuza maarufu Lamar.
Akizungumzia kundi hilo, Meninah anasema: “Kundi letu bado ni changa na tangu tuliunde tayari tumefanikiwa kuachia wimbo wa ‘On The Show’ sambamba na video ya wimbo huo. Lakini wiki tatu zilizopita tumeachia wimbo mwingine ‘Nifikirie’ na umepokelewa vizuri tu na mashabiki.”
Anasema kuwa hakuwahi kufahamiana na wasichana hao, bali aliunganishwa na Lamar aliyekuwa akitafuta vipaji kutoka kwa wasanii wanaojua kuzitumia sauti zao.
“Sikuwahi kufahamiana na Salma wala Nuru, ila Lamar ndiye aliyetuunganisha. Nashkuru, huko ninapata uzoefu mkubwa tu ambao nahisi nitaweza kuutumia sehemu yoyote. Hakuna kitu kizuri kama kufundishwa kazi na mtu aliyewaongoza wasanii wakubwa walioshika chati za juu hapa nchini.”
Licha ya kuwepo katika kundi hilo, msanii huyo amepewa uhuru wa kufanya kazi zake binafsi na hivi sasa ameonyesha kufanya kazi nzuri inayopendwa na wengi, hasa anapokuwa katika majukwaa.
“Nashkuru Mungu nina pumzi ndiyo sababu ninapata kazi nzuri. Alhamdulilah, naweza kupata mahitaji yangu binafsi kwani sasa simwombi tena mama pesa ya saluni, vocha na vitu vingine vidogo vidogo.”
Hata hivyo, Meninah hataki kuweka wazi ni kiasi gani cha fedha analipwa kwa shoo moja; “Kwa kweli siyo rahisi kusema, kwani huwa sipendi. Lakini shoo Napata, ila bado ni zile za chini huku, ila nina imani kwamba ipo siku nitafanya shoo kubwa zaidi nje ya nchil Ila, watu watambue kuwa Meninah siyo msanii ghali, bali ni makubaliano kati yangu na promota anayetaka kunipa kazi.”


Kwa sasa ameachia wimbo wake mpya unaokwenda kwa jina la Shaghala bhagala, unayofanya vizuri kwenye vituo mbalimbali vya redio, huku akiwa mbioni pia kutoa video ya wimbo huo chini ya prodyuza, Nash Designer.
Maisha yake halisi
Meninah ni mtoto wa tatu na wa mwisho kuzaliwa katika familia yake, huku Atick ‘Tik tik’ ambaye ndiye meneja wake akiwa mtoto wa kwanza kuzaliwa.
Msanii huyu ni mwanafunzi katika Shule Kuu ya Uandishi wa Habari ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (SJMC), akisomea Mawasiliano ya Umma.
Anasema kuwa licha ya kuwa na mambo mengi ya shughuli zake za kimuziki, bado anaweza kuhimili mikiki mikiki ya shule, pamoja na kutekeleza majukumu anayopangiwa na wazazi wake.
“Awali nilikuwa naona kama nataka kuchanganya mambo, lakini namshukuru Mungu kwani kwa sasa akili yangu imetulia. Mimi ni mwanamuziki nina majukumu mengi, kila wiki nakuwa na safari za mikoani kwa ajili ya shoo, bado natakiwa kuhudhuria darasani,” anasema.
Meninah anaongeza kuwa licha ya majukumu aliyonayo, anahakikisha anapata muda sahihi wa kusaidia wazazi wake katika kazi mbalimbali nyumbani. “Najipanga sana, nakabiliwa na mambo mengi,” anasema.
Aidha amewashukuru wazazi wake kwa kumuunga mkono katika kazi yake, vilevile anawaomba mashabiki kuipokea kazi yake.
Msanii huyo anayeishi na wazazi wake Mikocheni jijini Dar es Salaam, anasema kwamba licha ya yeye kuwa ni mwanamuziki anajitahidi kuwa katika maadili aliyofundishwa na wazazi wake, ikiwa ni pamoja na kujisitiri kimavazi.
source: Mwananchi