Monday 2 September 2013

Safari Hatua

                 
                                                           Tido Mhando 

Na Tido Mhando  (email the author)

Posted  Jumapili,Septemba1  2013  saa 13:36 PM
Kwa ufupi
Tido Mhando ni miongoni mwa watangazaji wa radio wakongwe Afrika ya Mashariki. Tangu mwishoni miaka ya 1960, jina la Tido Mhando limekuwa maarufu katika kanda hii kama mtangazaji wa muziki, michezo na baadaye habari na matukio.

Tido Mhando ni miongoni mwa watangazaji wa radio wakongwe Afrika ya Mashariki. Tangu mwishoni miaka ya 1960, jina la Tido Mhando limekuwa maarufu katika kanda hii kama mtangazaji wa muziki, michezo na baadaye habari na matukio. Ndani ya simulizi zake hizi za kila Jumapili, Tido anasimulia baadhi tu ya mambo aliyokutana nayo katika kipindi chake hicho. Jumapili iliyopita aliendelea kusimulia kuhusu maandalizi yake ya safari ya kwenda New Zealand kwenye michezo ya Nchi za Jumuiya ya Madola ya 1974. Maandalizi ambayo yaliingia dosari kiasi wakati ilipofahamika kwamba isingewezekana kwa RTD kutuma watangazaji wawili kwenye michezo hiyo kama ilivyokuwa imetarajiwa. SASA ENDELEA…
Haikuwa rahisi kupokea kauli ile ya Naibu Mkurugenzi, Sammy Mdee, kwamba kwa sababu ya uhaba wa fedha imelazimika mimi pekee niende kwenye michezo hiyo ya New Zealand badala ya kuambatana na mtangazaji mwenzangu Abdul Omar Masoud.
Tulikaa kimya kwa muda, lakini hatimaye, Masoud alinishika mkono na kunitakia kila la kheri. Tulijaribu kutafakari kuhusu uamuzi huo na tukakubaliana kwamba bila ya shaka uamuzi wa kunichagua mimi ulitokana na ukweli ya kwamba Masoud, mbali ya mchezo wa mpira wa miguu, alikuwa si mzoefu sana kwenye michezo mingine kama vile riadha na ngumi, tofauti na mimi.
Wakati tulipokuwa tukifanya mipango ya safari kwa pamoja tulikuwa tumezungumza mengi, siyo tu kuhusu jinsi ambavyo tungetangaza michezo hiyo, bali hata ambavyo tungevinjari pamoja huko Christchurch. Sasa yote haya yakawa yamesukumwa pembeni. Ikanibidi nianze kujipanga upya mwenyewe.
Nilipobakia peke yangu, niliwaza na kumsikitikia mwenzangu Masoud. Nilifahamu ni kwa jinsi gani tungeweza kuusisimua umma wa Watanzania kwa matangazo yetu ya pamoja, kwani sote tulikuwa wabunifu na wachangamfu. Lakini nikajisemea mwenyewe: “Yote kwa yote, lazima mambo yaendelee, tena kwa kasi ile ile.” Nikapania kufanya vizuri, japo peke yangu.
Kwa kweli, niliwashukuru sana viongozi wangu kwa kuwa na imani nami, hivyo nikadhamiria kutowaangusha hata kidogo. Lakini zaidi, nilimshukuru Mwenyezi Mungu maana kama uamuzi ungekuwa tofauti, ndoto yangu ya kuitumia safari hii kwa matayarisho ya harusi yangu ambayo ilikuwa imepangwa kufanyika mara tu baada ya kurejea, ingeingia dosari.
Hii ni kwa vile, katika kujipanga kwa maandalizi hayo, nilikuwa nimeiona safari hii kuwa nafasi nzuri ya kujinunulia vitu muhimu vya harusi, hasa mavazi yangu na ya mke wangu mtarajiwa.
Tulikuwa tumekubaliana na wazazi wangu kuwa pamoja na mambo mengine, wao wangelipa mahari ambayo yalikuwa ni Sh2,000 (Shilingi elfu mbili), kiasi cha kadiri sana hasa siku hizo, hasa kwa vile baba mkwe, Mzee Amos Mwaipopo ambaye alikuwa mzee mtaratibu sana, hakutaka makuu ya mahari makubwa na kwamba, mimi nami ningechuku gharama nyinginezo hasa hizo za mavazi yetu.
Kwa hiyo, nilipania kwenda kununua nguo za nguvu huko New Zealand, hasa za bi harusi, kwa kuwa pia nilikuwa tayari namfahamu vyema Mwangaza kwamba alikuwa mtu wa kupenda mavazi ambayo kwayo yalikuwa yakimkaa vizuri sana.
Katika desturi za mila za Kibondei, ilikuwa vilevile ni wajibu wangu mimi kama bwana harusi kuhakikisha ya kwamba namvalisha bi harusi, kwani wakati wa sherehe za kimila, tungetakiwa kutoka nje mara tatu, tukiwa tumevaa mavazi tofauti, na huku watu wakimwangalia zaidi bi hurusi. Kwa sababu hiyo, nilitarajia kuitumia safari hii vizuri kwa lengo hilo.
Kwa hakika siku zilikuwa zikienda haraka haraka sana na ghafla tukajikuta tumeingia kwenye mwaka mpya wa 1974, ikimaanisha ya kwamba siku za safari zilikuwa zimekaribia mno.
Kikosi cha wanamichezo wa Tanzania kilichokuwa kinakwenda kwenye michezo hii kilikuwa kikubwa kiasi. Kulikuwa na wanamichezo wengi wa riadha akina Suleiman Nyambui, Mwinga Mwanjala, Nzael Kyomo, Norman Chihota na nyota Filbert Bayi na wengine wengi wazuri sana.
Pia walikuwamo wachapa masumbwi wazuri tu kama vile Habibu Kinyogoli na Emmanuel Mlundwa. Hata tulikuwa na waendeshaji wa baiskeli waliokuwa na uhodari wa kushindana kwa kiwango cha juu kwenye mashindano kama haya ya kimataifa ikiwa ni pamoja na George Mulamula. Halikadhalika tulikuwa na wachezaji wa mpira wa meza (table tennis). Kwa kweli ilikuwa timu iliyosheheni vyema.
Wote hawa walipewa nafasi nzuri ya kufanya mazoezi ya kweli kweli huku Serikali ikiwa mstari wa mbele wa kugharimia maandalizi haya vyema. Vilevile, wale wote ambao tulikuwa kwenye safari hii, ikiwa ni pamoja na sisi waandishi wa habari, tulipatiwa sare maalumu za kupendeza. Mwandishi mwingine wa habari kwenye safari hii alikuwa ni Stephen Rweikiza aliyekuwa akiandikia gazeti la Daily News.
Tuliondoka sote kwa pamoja kuelekea New Zealand kwa kutumia ndege ya Shirika la Ndege la Afrika Mshariki (East African Airways) hadi Port Luis, Mauritius. Tulilala kwenye kisiwa hiki maarufu kwa zao la miwa kwa usiku mmoja.
Nakumbuka sana wakati tulipokuwa tukielekea kwenye hoteli hiyo tuliyopangiwa kulala tukipita kwenye ekari na ekari za mashamba makubwa sana ya miwa, huku tukipishana na viberenge vingi vilivyobeba malundo ya miwa iliyokatwa kupelekwa kwenye vinu vya kutengenezea sukari.
Tuliondoka Mauritius mapema asubuhi sana kwa ndege kubwa zaidi ya Shirika la Ndege la Qantas kwa safari ndefu ya saa kumi na ushei kuivuka Bahari ya Pacific. Ilikuwa vizuri kwamba tulikuwa kwenye kundi la watu wengi maana tuliweza kuchangamshana kwa kucheza michezo kadhaa midogo midogo mle ndani ya ndege kama vile karata, ili kupitisha muda maana hii ilikuwa safari ya kuchosha sana hii.
Tuliwasili mji wa Perth, Australia, kiza kikiwa kimeingia. Tulikuwa tumesimama kwa muda tu hapo kubadilisha ndege ya kutupeleka Christchurch. Nikiwa kiwanjani hapo nilianza kuona hali ya maisha ilivyo tofauti. Niliona maendeleo makubwa ya miundombinu ya kisasa zaidi.
Baada ya muda wa saa mbili hivi, tuliondoka Perth na ndege ndogo kiasi ya shirika hilo hilo la Qantas kwa mkondo wa mwisho wa safari yetu hii, tukawasili New Zealand kiasi cha saa tano usiku tukiwa tumechoka sana.
Hata hivyo nilifurahi hatimaye kuwasili nchini New Zealand, kwani baada ya miezi kama miwili ya kusubiri na kufanya maandalizi mbalimbali sasa nikawa nimetua kwenye hii ya nchi ya mbali sana. Maili elfu kadhaa kutoka nyumbani Tanzania. Kwa kweli sikuwa nimetarajia kwamba siku moja ningeweza kufika mahali kama huko, na mapema kiasi hicho kwenye maisha yangu ya kikazi.
Lakini pia nilifahamu kwamba nilikuwa nakabiliwa na changamoto pamoja na kazi kubwa mbele yangu na hasa kwa kuwa sasa nilikuwa peke yangu. Kabla ya kuondoka, nilikuwa nimefanya maandalizi mazuri ili kuhakikisha kuwa natekeleza kazi yangu kwa kiwango cha juu.
Nilihakikisha ya kwamba nilikuwa nimekusanya kila kitu ambacho kingeniwezesha kutoa habari kwa usahihi mkubwa. Nilisoma vitabu na majarida mbalimbali kuhusu Michezo ya Jumuiya za Madola. Nilifanya juhudi za kuwafahamu wanamichezo mbalimbali maarufu watakaokuwepo kwenye michezo hiyo na kuhakikisha nawafahamu vizuri sana wanamichezo wetu.
Halikadhalika, nilipata maelezo na maelekezo ya kutosha ya jinsi nitakavyokuwa ninatuma habari za michezo hiyo. Tayari kulikuwa kumefanyika mawasiliano ya kutosha baina ya RTD na wasimamizi wa matangazo ya radio ya mashindano haya ambapo nilikuwa nimepangiwa muda na studio maalumu wa kurusha matangazo yangu hayo.
Nilikuwa nimepangiwa kutuma kipindi maalumu cha muda wa dakika 15 kila siku za majuma mawili ya michezo hiyo, nikifahamisha yote yale muhimu na ya kusisimua ambayo yangekuwa yametokea siku nzima kwenye viwanja mbalimbali.

Ili kutia ladha katika matangazo yangu hayo, nilitafuta wimbo wangu maalumu, (signature tune) ambayo ningekuwa ninaicheza kila wakati wa kufungua na kufunga kwa ripoti hizo. Niliutafuta wimbo huo kwa umakini mkubwa, nikishinda kwa muda mrefu kwenye maktaba hadi nilipofanikiwa kupata wimbo mzuri wa ala tupu uliokuwa wa kusisimua, wenye mahadhi ya ngoma za kienyeji, uliokuwa umepigwa na bendi ya Jeshi la Tanzania.
Kwa hakika, nilikuwa nimejipanga vizuri. Lakini sasa tukiwa bado hapo kwenye uwanja wa ndege, baaada ya kukamilisha taratibu zote za uhamiaji ambazo zilifanyika kwa haraka sana kwa sababu tulikuwa wageni mashuhuri, hali ya taharuki ikanitokea baada ya kukosa kulipata sanduku langu.
Kama desturi ya safari za ndege, nakumbuka hii ilikuwa safari yangu ya kwanza ndefu, nililitoa sanduku hilo pale uwanja wa ndege wa Dar na kama wengine wote tukafahamishwa ya kwamba tusiwe na shaka yoyote tungepata masanduku yetu hayo mwishoni kabisa mwa safari.
Sasa wakati wenzangu wote walifanikiwa kupata masanduku yao, miye langu halikupatikana hata baada ya wasimamizi wa ndege na uwanja kufanya juhudi kubwa ya kulitafuta. Kikawa kisanga kingine. Nikawa nawaza na kuwazua, Nikaona hii balaa.
Hata hivyo maofisa wa ndege wa Qantas walinitoa shaka kwa kunifahamisha ya kwamba wangenipatia kiasi kizuri tu cha fedha kuweza kununua nguo chache za kutumia huku wao wakiendelea kulitafuta sanduku hilo.
Nilifarijika na kuondoka na wenzangu wote kuelekea hoteli tuliokuwa tumepangiwa kufikia sisi waandishi wa habari wakati wachezaji na viongozi wao walikuwa wanapelekwa kwenye kijiji maalumu cha wanamichezo.
Tulipita maeneo mengi mazuri ya mji huo wa Christchurch nikavutiwa nao sana. Mji ulikuwa umepangwa na kupangika ukiwa na vivutio vingi vinavyokufanya upende kuishi humo. Lakini pamoja na yote hayo, nilijua sasa kazi ndiyo imeanza.
INAENDELEA JUMAPILI IJAYO...

source: Mwananchi