Monday 2 September 2013

Pacha aliyetenganishwa MOI sasa aanza kunyonya


Na Vicky Kimaro, Mwananchi  (email the author)

Posted  Agosti31  2013  saa 8:58 AM
Kwa ufupi
Pacha huyo alizaliwa Agosti 18 Zanzibar akiwa ameungana na kiwiliwili na baadaye alihamishiwa Muhimbili.


Dar es Salaam. Siku moja baada ya jopo la madaktari bingwa wa upasuaji kutoka Taasisi ya Mifupa Muhimbili (Moi) kwa kushirikiana na wale wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) kuokoa maisha ya mtoto aliyekuwa ameungana na kiwiliwili cha pacha mwenzake, mama wa mtoto huyo, Pili Hija (24), amesema hakutegemea kama mtoto wake angepona.
Hija alitoa kauli hiyo jana alipozungumza na Mwananchi Jumamosi na kudai kuwa, kabla alikata tamaa akidhani atampoteza mtoto wake, lakini kwa nguvu za Mungu madaktari wamemwokoa na ameanza kunyonya.
“Sina cha kuwalipa madaktari zaidi nawaombea kwa Mwenyezi Mungu, sikutegemea kama leo hii ningekuwa na mwanangu namnyonyesha, nilishakata tamaa na kumkabidhi Mungu, yeye ndiyo amenipa, basi atende atakavyo. Nashukuru mwanangu anaendelea vizuri,” alisema Hija na kuongeza huku akitabasamu:
“Bibi yake mzaa baba na shangazi yake walikuja jana usiku (juzi), wamempa jina la Kudra, kwa vile ni Kudra za Mwenyezi Mungu pekee ndiyo zimemweka hai mpaka leo.”
Alisema anashukuru mtoto wake ameshaanza kunyonya vizuri, pia jana asubuhi alipata choo kikubwa na kuwaasa wazazi wenye watoto walemavu kuacha kuwanyanyapaa kwa kuwaficha.
Daktari Bingwa wa Ubongo na Uti wa Mgongo ambaye aliongoza jopo la madaktari saba katika upasuaji huo, Dk Hamis Shaaban, alisema kiwiliwili cha mtoto ambaye hakukamilika licha ya kutokuwa na kichwa na macho, hakikuwa na moyo, figo, tumbo na maini.
Dk Shaaban alisema kilikuwa na uti wa mgongo na kwamba, huenda tatizo hilo limesababishwa na upungufu wa madini ya Folic Acid ambayo mama alitakiwa kupata kipindi cha ujauzito.
Hata hivyo, Pili alipoulizwa kuhusu kutumia madini hayo kipindi cha ujauzito alisema: “Nilipokuwa na mimba nilikuwa naumwa umwa sana, nikaanza klinic ikiwa na miezi mitatu, nilikutwa sina damu kuna dawa nilipewa za kuongeza damu nikazitumia zilipoisha nikarudi tena, ikawa imeongezeka nikambiwa nisitumie tena.”
Msemaji wa Moi, Jumaa Almas, alisema mtoto anaendelea na ananyonya vizuri, bado yupo chini ya uangalizi maalum (ICU) hadi afya yake itakapoimarika.

source:Mwananchi