Saturday 14 September 2013

HATARI: Samaki hatari waingizwa nchini

Samaki wabovu walionunuliwa kutoka katika soko la Feri jijini Dar es Salaam juzi. 



Posted  Septemba14  2013  saa 6:46 AM
Kwa ufupi
Samaki hao kutoka Yemen, Dubai, China na Japan, wanaoingizwa nchini wakiwa wameganda kwenye barafu, wengi huharibika muda mfupi baada ya barafu kuyeyuka au baada ya kununuliwa.


Dar es Salaam. Afya za Watanzania ziko shakani kutokana na kuwapo kwa biashara ya kuingiza samaki kutoka nje ya nchi, wanaodaiwa kuharibika na kuuzwa katika la Soko la Feri jijini Dar es Salaam.
Samaki hao kutoka Yemen, Dubai, China na Japan, wanaoingizwa nchini wakiwa wameganda kwenye barafu, wengi huharibika muda mfupi baada ya barafu kuyeyuka au baada ya kununuliwa.
Uchunguzi wa gazeti hili umegundua kuwa samaki hao huletwa nchini kutafutiwa soko baada ya kukaa kwenye majokofu kwa muda mrefu huko wanakotoka, kiasi cha kuelekea kuharibika.
Ili wasiharibike, samaki hao aina ya Marckerel hukaangwa hadi wakauke. Uchunguzi zaidi umebaini kuwa wanunuzi wake wakuu ni wafanyabiashara wa chakula wakiwamo wamiliki wa migahawa na Mama Lishe wanaofanya shughuli zao katika miji ya Dar es Salaam, Pwani, Morogoro na Dodoma.
Samaki hao wanauzwa kwa bei ya chini ambayo ni Sh38,000 kwa boksi lenye uzito wa kilo 15, ikilinganishwa na wanaovuliwa hapa nchini ambao bei yake ni Sh60,000, kwa uzito huohuo.
Inaelezwa kuwa samaki hao baadhi yake ni wale ambao wamekwisha muda wake wa kutumika katika nchi hizo, hivyo kuingizwa nchini kutafutiwa soko.
Gazeti hili lilifika katika soko hilo kwa siku mbili na kushuhudia samaki hao wakiuzwa kwa wingi, huku wauzaji wakihimizwa wateja wao kuwahi kuwakaanga au kuwaweka kwenye jokofu.
Gazeti hili pia lilinunua boksi moja la samaki hao lenye uzito wa kilo 15 kwa Sh38,000, lakini lilipodai kupewa stakabadhi wauzaji walisema: “Hatuna stakabadhi ya kukupa ndugu yangu,” alisema muuzaji.
Baada ya kuwasafirisha kutoka Soko la Feri hadi ofisi za gazeti hili zilizopo Tabata Reli, Barabara ya Mandela kwa muda wa saa moja, tayari walikuwa wameharibika.
Baadhi ya samaki hao walianza kuoza huku wengine wakiwa wamelegea tofauti na samaki wa kawaida. Baada ya saa nne kupita, samaki hao waliharibika na kuanza kutoa harufu mbaya.
Dk Raymond Mwenekano wa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, anayataja madhara ya ulaji wa samaki wa aina hiyo kuwa ni kupata magonjwa kama vile kansa ya utumbo, mwili kuwasha, kubabuka na vidonda mwilini.
“Madhara yake ni makubwa, ndiyo maana siku zote tunasisitiza kula vyakula visivyokaa sana kwani vingine vimehifadhiwa kwa dawa na wanaofanya hivi ni wafanyabiashara kwa faida yao,” alisema Dk Mwenekano.

Daktari huyo alisema pia yapo madhara ya muda mfupi ambayo ni mtu aliyekula samaki wa aina hiyo kuharisha na kutapika muda mfupi baada ya kula.
Mamlaka husika
Ofisa Afya katika Soko la Feri, Barnabas Hanje alithibitisha kuwepo katika soko hilo, samaki wabovu wanaotoka nje ya nchi na kwamba ofisi yake imekuwa ikipokea malalamiko mengi kuhusu suala hilo.
Hanje ambaye pia alitajwa kuwa ni Mwakilishi wa Mamlaka ya Chakula na Dawa Tanzania (TFDA) katika soko hilo, alisema kesi zinawahusu wanunuzi wanaodai warejeshewe fedha au kubadilishiwa samaki, baada ya wale waliowanunua kuharibika haraka hata kabla hawajatoka sokoni hapo.
Alifafanua kuwa baadhi ya kesi hupata ufumbuzi baada ya waliouza samaki wabovu kukubali kurejesha fedha kwa wahusika na kwamba kwa pale mwagizaji wa jumla anapokataa kurejesha fedha kesi hizo hupelekwa mahakamani.
“Sina idadi kamili ya kesi, lakini kesi kama hizo ni nyingi na baadhi yake tuliposhindwa kuwapatanisha watu wawili mnunuzi na muuzaji tuliwaambia waende mahakamani, lakini nakiri ni kweli jambo kama hilo lipo,” alisema Hanje.
Ofisa Uvuvi wa Manispaa ya Ilala, Msongo Songoro alisema wamekuwa wakipata changamoto nyingi kuhusiana na suala hilo ndiyo maana wameanza mchakato wa kutambua kampuni zote zinazoingiza katika Soko la Feri samaki kutoka nje ya nchi.
Alisema hadi sasa wamebaini kuwapo kwa kampuni 20 na kati ya hizo ni sita pekee ambazo zimewasilisha uthibitisho wa kufuata sheria pale wanapoingiza shehena ya samaki nchini. Songoro aliongeza kuwa karibu tani moja na nusu ya samaki hao kutoka nje wanauzwa kila siku katika Soko la Feri.
“Niliwahi kupata kesi kama hizo ambapo nilichukulia kama changamoto na kuanza kufanya hiki ninachokifanya sasa na hadi sasa ni kampuni sita pekee ambazo wameniletea vibali vyao vinavyoonyesha uhalali wa kuagiza shehena ya samaki kutoka nje kati ya kampuni 20 ambazo zinaagiza,”alisema Songoro.
Songoro alivitaja vitu ambavyo kila kampuni inatakiwa kuviwasilisha kwao kuwa ni pamoja na Cheti cha Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Cheti cha Usajili wa kampuni, Cheti cha TFDA, leseni ya biashara na vibali vyote vinavyoruhusu kuingiza samaki nchini.
Ofisa Maliasili wa Manispaa ya Ilala, Charles Seche, alisema hatua walizochukua ni mwanzo lakini lengo ni kuondosha bidhaa zote zisizo na ubora katika soko hilo.
Ofisa Uhusiano wa TFDA, Gaudencia Simwanza alipoulizwa alisema hafahamu kuhusu uwepo wa samaki wabovu na kuahidi kwamba angekwenda kulijadili na wahusika.

Alimtaka mwandishi wa habari amwambie samaki hao wameanza kuingia lini nchini, wanatoka nchini gani na wanaitwaje, ili aweze kuwasiliana na wahusika wa idara ya chakula.
“Wewe ndiyo unaniambia nitaiwasilisha kwenye idara ya wahusika wa chakula moja kwa moja waifanyie kazi na baada ya kukamilisha uchunguzi nitakupa taarifa,” alisema Simwanza.
Alipohojiwa baada siku moja, Simwanza alisema jukumu la TFDA ni kuangalia mzigo ambao unaingizwa kwa wingi na hii ni baada ya kupokea sampuli na kuridhishwa nao, kisha hutoa kibali kwa ajili ya kuruhusu uingizwe.
“Kazi yetu sisi ni hiyo kwa mzigo uliopo sokoni hasa wa vyakula muhusika mkuu ambaye tunafanya naye kazi kwa karibu ni ofisa afya wa soko ambaye ndiye ana wajibu wa kukagua mzigo na kuangalia una tatizo gani,”alisema Simwanza.
Simwanza alifafanua kuwa hata wanapotoa kibali cha kuingiza mzigo siyo mwisho, kwani unapowasili huwa unafanyiwa ukaguzi mwingine uwapo bandarini na ukigundulika una matatizo unazuiliwa.
Samaki bado wapo
Hata hivyo, uchunguzi uliofanywa unaonyesha kuwa pamoja na kufanya ukaguzi, samaki wasiofaa wanaendelea kuingizwa katika soko hilo.
Mmoja wa wachuuzi wa samaki katika soko hilo (ambaye hakupenda kutaja jina lake gazetini), aliliambia gazeti hili kuwa samaki hao huuzwa kwa bei ya chini ikilinganishwa na wanaovuliwa nchini.
“Siyo bure, huwezi kusafirisha samaki kutoka Uarabuni kuja kuuza nchini kwa bei ya chini, je wewe unanunua kwa bei gani?” alihoji na kusema ndiyo maana wengi wa samaki hawa wameharibika.
Alisema kama Serikali haitakuwa makini basi Watanzania wanaweza kujikuta wanapata magonjwa mengi kutokana na kugeuzwa dampo la vyakula visivyofaa.
Uchunguzi unaonyesha kuwa baada ya kuingizwa nchini shehena ya samaki hao wakiwa katika makontena ya barafu, hupelekwa kuuzwa katika soko hilo wakiwa wamehifadhiwa kwenye chumba cha barafu.
 
Baadhi ya wateja wanapowatoa katika makasha waliyofungiwa na kuwaosha, huharibika kabla hawajafika nyumbani. Baadhi ya wachuuzi wanasema samaki hao hukosa soko kipindi ambacho samaki wanakuwa wakipatikana kwa wingi wa nchini.

Mmoja wa wachuuzi hao, Hamisi Ally alisema, “Niliwahi kupata taabu niliponunua samaki hao ili nikauze, maana wakati nagawana na mwenzangu walikuwa wanatoa harufu kali na tulipowachunguza walikuwa wameharibika kabisa.”
Mwingine ni Mwajuma Jumbe ambaye alisema, aliwahi kupata bahati mbaya ya kununua samaki hao bila kujua na alipowauza alipata malalamiko kutoka kwa wateja wake ambao walisema amewauzia makapi kwa maana ya samaki kukosa ladha.
“Mm! bora nisote ninunue kidogokidogo hadi nijaze ndoo kuliko kununua hao ‘kamongo’, waliwahi kukata msingi (mtaji) wangu maana nilinunua na baada ya muda wakaharibika. Hao samaki wanataka uwaandae wakiwa na barafu. Naona shida kununua kitu halafu kinipeleke puta,” alisema Jumbe.
Mmoja wa wavuvi wa soko la Feri, Juma Abdul (siyo jina lake halisi) alisema samaki hao hununuliwa na wachuuzi kutoka maeneo mbalimbali ya jiji kwa kuwa bei yake ni ya chini, ikilinganishwa na samaki wengine.
“Ukitaka kutambua hilo njoo asubuhi utashuhudia kila kitu, samaki hawa si salama na wapo wavuvi ambao wamefikisha malalamiko yao kwa uongozi wa soko,” alisema.
Alisema kuwa samaki hao mbali na kuharibika ndani ya muda mfupi, ukiwala wanakuwa hawana ladha halisi ya samaki na kwamba ili uwauze kiurahisi ni lazima uwakaange wakauke sana.
Waagizaji wa samaki
Kampuni moja ambayo inaingiza samaki hao kutoka nje ya nchi ni Alpha Crust, ambayo Ofisa wake wa Rasilimaliwatu, Elton Kachele alisema hawajawahi kupata malalamiko ya samaki kuharibika muda mfupi baada ya kununuliwa.
Kachele alisema kuna uwezekano samaki huharibika kutokana na jinsi wanavyohifadhiwa baada ya kutoka mikononi mwao, kwani wao huwahifadhi vizuri na kwamba hata samaki wa kawaida kama hakutunzwa vizuri huharibika.
Kachele aliongeza kuwa samaki wao kabla ya kuingia sokoni hupita katika Mamlaka husika ikiwamo TFDA na TBS, ili kuthibitisha kama wanaweza kuingia sokoni na kuliwa.
“Hata mwaka jana tulipata msukosuko baada ya kuwepo kwa shutuma kama hizo na Wizara ya Afya pamoja na TFDA, walikuja hapa kukagua na wakaona hakuna tatizo sasa kama bado linaendelea ni huko nje lakini hapa kwetu kila kitu kipo safi,” alisema Kachele.
Alisema samaki wao wanaagizwa kutoka Yemen na Japan, na baada ya kupata malalamiko hayo aliwahi kwenda hadi kwenye Soko la Feri kuangalia kwenye vyumba vya kuhifadhia na kukuta kila kitu kipo sawa.

Mkurugenzi wa kampuni hiyo aliyejitambulisha kwa jina la Vedagiri, alisema anachojua kabla ya kuuza samaki wanapitia kwenye taratibu zote za Serikali ikiwemo ukaguzi wa kina kutoka kwa mamlaka husika.
“Hao ambao wamepata samaki wabovu na wanaamini wametoka kwangu walete ushahidi, lakini mimi ninachojua mamlaka husika zimethibitisha kuwa wapo safi na ndiyo maana nauza na watu wanakula,” alisema Vedagiri.
Juni, 2009 uongozi wa Soko la Feri ulikamata tani moja ya samaki waliovuliwa kwa kutumia baruti ambao hawafai kwa matumizi ya binadamu wakiwa wanauzwa sokoni hapo.
Agosti 2011,
Jeshi la polisi lilikamata tani 123.908 za samaki aina ya Marckerel kutoka Japan zikituhumiwa kuwa zilikuwa na mionzi ya nyuklia kutokana na nchi hiyo kupata ajali ya kinu cha nyuklia kuvuja.
Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii iliiagiza Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) kufanya ukaguzi na kuhakikisha kuwa samaki hao wanazuiliwa ili wasitumiwe.
Hata hivyo, baadaye TFDA ilitoa taarifa kuwa samaki hao hakuwa wamechafuliwa na mionzi ya nyuklia kutoka Japan.
Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Dk David Mathayo David alipoulizwa kuhusu samaki hao wabovu alijibu kwa kifupi: “Nipo njiani naendesha hivyo siwezi kulitolea ufafanuzi suala hilo.”
Kwa upande wake Naibu Waziri wa Wizara hiyo, Benedict Ngalama Ole-Nangoro, yeye alipoulizwa alimtaka mwandishi ampelekee maswali kwa maandishi wayafanyie kazi na kuyatolea ufafanuzi.
SOURCE: MWANANCHI