Wednesday 23 October 2013

Wavamia kanisa waua, wajeruhi


Na Frederick Katulanda, Mwananchi

Posted  Jumatano,Oktoba23  2013  saa 24:0 AM
Kwa ufupi

Kwa mujibu wa Askofu Eliabu Sentozi, alisema kwa mwonekano na sura ya tukio hilo, halionyeshi kuwa na nia ya ujambazi kutokana na wavamizi hao kutokuiba chochote ndani ya kanisa hilo na hivyo kuitaka Serikali kuangalia kwa makini mfululizo wa matukio haya yanayotokea kanisani.

Mwanza. Muumini mmoja wa Kanisa la Gilgal Christian ameuawa na wengine wawili wamejeruhiwa vibaya kwa kukatwa na mapanga sehemu mbalimbali mwilini baada ya watu wasiofahamika kuvamia kanisa hilo usiku wa manane kwa lengo na nia isiyojulikana.
Tukio hilo lilitokea Oktoba 22 mwaka huu saa 7 usiku, eneo la Pasiansi wilayani Ilemela mkoani Mwanza. Aliyeuawa katika tukio hilo lililowasikitisha wengi, ametajwa kuwa ni Elias Meshack.

Aidha, upande wa waliojeruhiwa wametajwa kuwa ni Elias Msakuzi ambaye alitibiwa na kurejea nyumbani baada ya kujeruhiwa kichwani pamoja na Tumsifu Pungu ambaye bado amelazwa Hospitali ya Rufaa ya Bugando akiendelea kupata matibabu na hali yake imeelezwa kuendelea vizuri.
Kwa mujibu wa Askofu Eliabu Sentozi, alisema kwa mwonekano na sura ya tukio hilo, halionyeshi kuwa na nia ya ujambazi kutokana na wavamizi hao kutokuiba chochote ndani ya kanisa hilo na hivyo kuitaka Serikali kuangalia kwa makini mfululizo wa matukio haya yanayotokea kanisani.

“Sidhani kama hili ni tukio la ujambazi, maana malengo ya jambazi huwa ni kusaka fedha ama vitu sasa hapa hakuna kilichoibwa,” alisema.
Alisema kinachowafanya kuamini kwamba wahusika hawakuwa na nia ya wizi ni kutokana na kutochukua kitu chocote ingawa ndani ya kanisa kulikuwa na vitu vingi vyenye thamani.
Kamanda wa Polisi mkoani Mwanza, Ernest Mangu amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kusema kwa sasa jeshi lake limeanza uchunguzi wa tukio hilo.
“Nitatoa ufafanuzi baadaye, kwa sasa tupeni nafasi ya kuchunguza hili jambo. Hatuwezi kujua nia hasa ilikuwa nini, lakini baada ya uchunguzi taarifa zitatolewa,” alieleza kamanda huyo wa polisi.
Mpaka sasa bado hakuna mtu yeyote aliyetiwa nguvuni.

SOURCE: MWANANCHI