Friday 1 November 2013

Watahadharisha Tanzania kujitoa EAC

Dar es Salaam. Siku moja baada ya Serikali kuweka msimamo wake baada ya nchi za Kenya, Uganda na Rwanda kutoihusisha Tanzania katika mambo yanayohusu Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), wasomi nchini wamesema Jumuiya hiyo inaendeshwa kwa uamuzi wa wanasiasa, wananchi hawashirikishwi katika uamuzi.
Wamesema mara nyingi nchi zilizopo katika umoja zinatupiana maneno baada ya kutofautiana kwa viongozi wake wa kisiasa.
Walisema sababu za kujitoa zilizotolewa na Tanzania hazina mantiki. Juzi Serikali kupitia kwa Waziri wake wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta ilieleza msimamo wake ikiwa ni pamoja na kutohudhuria mikutano ya jumuiya hiyo yenye ajenda ambazo nchi hizo tatu zimekwishaweka msimamo wa peke yao.
Nchi za Rwanda, Uganda na Kenya zimeanzisha ushirikiano wa pamoja katika maeneo ya miundombinu, biashara na viza ya pamoja na mara nyingi viongozi wakuu wa nchi hizo wamekuwa wakifanya mikutano bila kuzihusisha Tanzania na Burundi
.
Wakizungumza na gazeti hili kwa nyakati tofauti jana, Mhadhiri wa Chuo Kikuu Dar es Salaam, Bashiru Ally, alihoji, “Uamuzi wa Tanzania kujitoa katika EAC unafanywa kwa niaba ya wananchi au wanasiasa?”
Alisema mkataba wa jumuiya hiyo unaeleza kuwa jumuiya ni mali ya watu wa Afrika Mashariki. Mhadhiri mwingine wa chuo hicho, Dk Kitila Mkumbo alisema sababu zinazoelezwa na Serikali hazina mantiki.
“Binafsi naona jumuiya hii ni ya wanasiasa. Sidhani kama Serikali yetu imewahi kuwaeleza wananchi kuwa Tanzania inafaidika vipi na jumuiya hii.”
Mhadhiri wa Chuo Kikuu Huria, Emmanuel Mallya alisema kuwa, msingi wa jumuiya hiyo ni kushirikiana kwa mambo yenye masilahi kwa nchi husika.
“Kama Tanzania inaona nchi nyingine zinataka kushirikiana nayo katika mambo ambayo yenyewe haijayaafiki sidhani kama litakuwa jambo baya kujitoa,” alisema

SOURCE: MWANANCHI