Friday 18 October 2013

Mkapa alivyowezesha NMG kuwekeza Mwananchi

Rais Mstaafu, Benjamin Mkapa PICHA|MAKTABA 
Na Mwandishi Wetu, Mwananchi

Posted  Ijumaa,Oktoba18  2013  saa 24:0 AM
Kwa ufupi
Lengo lilikuwa ni kuwahabarisha Watanzania kwa misingi ya taaluma na weledi.

Dar es Salaam. Rais Mstaafu, Benjamin Mkapa ,ndiye aliyeialika Kampuni ya Nation Media Group (NMG) ya Kenya, kuja kuwekeza katika sekta ya habari hapa nchini, imeelezwa.
Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya NMG, Wilfred Kiboro alisema juzi usiku jijini Dar es Salaam kuwa, baada ya kupata wito huo, NMG iliamua kuja kuwekeza Tanzania kwa kununua hisa katika Kampuni ya Mwananchi Communications Ltd (MCL).
“Nakumbuka wakati huo nikiwa Ofisa Mtendaji Mkuu wa NMG, niliambatana na aliyekuwa Mwenyekiti wa Bodi na tulikwenda kumwona Rais Mkapa kule Arusha na katika mazungumzo yetu, alitualika tuje kuwekeza nchini,” alisema Kiboro alipokuwa akizungumza kwenye hafla ya MCL na wadau wake juzi.
Alisema: “Rais Mkapa alituambia angependa Watanzania wahabarishwe katika misingi ya taaluma na weledi kwa kupewa taarifa zisizoegemea upande mmoja na za kweli, tumefanya kazi hii kwa ufanisi katika safari ndefu ambayo tumekuwa nayo”.
Kiboro alisema uwekezaji kupitia MCL umechangia kwa kiasi kikubwa katika uchumi wa nchi kupitia kodi mbalimbali zinazolipwa na kwamba mchango huo, hauna maana kwamba kampuni hiyo inabeba ajenda yoyote kutoka Kenya.
“Hatuna ajenda yoyote ya Kenya hapa Tanzania, na pengine ajenda tuliyonayo ni moja tu nayo ni kuimarisha ushirikiano katika Jumuiya ya Afrika Mashariki,” alisema Kiboro.
“Kwa hiyo, kama alivyosema Mwenyekiti wa Bodi ya MCL, hakuna kumbukumbu zozote zinazoonyesha kwamba MCL inaendeshwa kwa maelekezo au maagizo kutoka Kenya, hatujawahi kufanya hivyo na wala hatuna mpango wa kufanya hivyo,” alisisitiza.
Kiboro pia alizungumzia kufungiwa kwa Gazeti la Mwananchi kwa muda wa wiki mbili na kuweka bayana kwamba, hatua hiyo ilikuwa na athari kubwa kwa watu ambao kwa namna moja au nyingine wana uhusiano na gazeti hili.
“Pengine ni wito wetu kwa Serikali kwamba kunapokuwa na tatizo kwenye vyombo vya habari ifuate mkondo wa kimahakama kuliko utaratibu unaofanya Serikali iwe mlalamikaji, mwendesha mashtaka, shahidi na hata mtoa hukumu,” alisisitiza.
Mwenyekiti wa MCL:
Mapema Mwenyekiti wa Bodi ya MCL, Zuhura Muro, alisema Serikali ni kama ilifanya kuvizia wakati ikichukua hatua za kulifungia Mwananchi kutokana na vitendo vilivyoambatana na kufungiwa huko

“Ni kama walituvizia, wale mliopita jeshini mtakuwa mnafahamu vizuri uviziaji, maana hata katika mkutano wa waandishi wa habari ulioitishwa ili kutangaza Mwananchi limefungiwa, waandishi wa habari wa Mwananchi hawakualikwa wala wa Gazeti la The Citizen hawakualikwa,” alisema Muro.
Alisema alipigiwa simu na watu waliomweleza kuwa gazeti limefungiwa baada ya kuona taarifa kwenye mitandao ya kijamii na alipokwenda kwenye Mtandao wa Jamii Forums, alikuta taarifa ya Gazeti la Serikali (GN) inayoeleza kufungiwa kwa Mwananchi.
“Baada ya kuthibitisha kweli ni taarifa ya Serikali, nilitoa maelekezo gazeti lisichapishwe, pamoja na hatua hiyo bado usiku ule unamwona Ofisa wa Serikali akizungumza kwenye televisheni Mwananchi ni wakaidi, unajiuliza huu ni ukaidi upi,” alisema.
“Taarifa ya kufungiwa ilitolewa kwenye Gazeti la Serikali la Septemba 27, lakini mkutano wa waandishi wa habari uliitishwa Septemba 28 wakati gazeti letu lipo mitaani, lakini sisi tuliletewa taarifa rasmi ya kufungiwa kwa maandishi, Jumatatu Septemba 30, saa 8:00 mchana, ndiyo maana nasema sikuelewa lugha kwamba Mwananchi ni wakaidi,” alisisitiza Muro.
Alisema pamoja na maumivu yaliyotokana na kufungiwa huko, MCL itaendelea kutimiza wajibu wake kwa umma kama ambavyo imekuwa ikifanya.
“Tumefanya mengi, tumekuwa na mfululizo wa makala kuhusu miaka 50 ya uhuru wa nchi yetu, tumeanza kufanya hivyo kwa ajili ya miaka 50 ya Muungano, tunaandika kitabu kwa ajili ya kutunza kumbukumbu, sasa hapo pengine mtu atuambie ni uzalendo wa aina gani tunaopaswa kuwa nao,”alihoji Muro.
Mmoja wa waliohudhuria hafla hiyo, Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba, alisema mchakato wa Katiba Mpya unaoendelea nchini unaweza kusaidia kuondoa kile kinachoonekana kuwa ni sheria kandamizi.

SOURCE: MWANANCHI