Sunday 13 October 2013

Mvurugano Afrika Mashariki washika kasi

13th October 2013
Mvurugano kwenye Jumuiya ya nchi za Afrika Mashariki (EAC) unazidi kushika kasi, baada ya muungano wa kimsimamo wa nchi za Tanzania na Burundi kuanza kuleta tishio kwa nchi tatu wanachama wa jumuiya hiyo zinazodaiwa kuanzisha mchakato wa siri wa kijitenga.
Hofu hiyo imetokana na tamko la hivi karibuni lililotolewa na nchi ya Burundi kwamba inaunga mkono msimamo wa Tanzania kwa kutotambua `utatu' ulioanzishwa na nchi za Uganda, Kenya na Rwanda.


Habari kutoka vyanzo vya kuaminika, vinasema tayari viongozi wa nchi ya Rwanda wameanza kuwatuhumu viongozi wa Burundi kwa kitendo hicho, wakieleza kinavunja udugu uliokuwapo kati ya wananchi wa nchi hizo mbili.

Wiki iliyopita Waziri wa Afrika Mashariki wa Burundi, Leontine Nzeyimana, wakati akizungumza na NIPASHE alisema wazi nchi yake haitambui mikutano yote iliyofanywa na viongozi wa nchi hizo kwa sababu imefanyika kinyume na makubaliano ya EAC.

Waziri Nzeyimana aliweka wazi kwamba hata miradi iliyokubaliwa kuanzishwa wakati wa mikutano hiyo ni batili na kamwe haitaingizwa kwenye jumuiya kutokana na kutoshirikishwa kwa nchi zote tano wanachama.

Kutolewa kwa kauli hiyo ilionekana kuwa mwiba mkali kwa nchi hizo, ambapo haraka viongozi wa Rwanda waliwasiliana na Burundi na kuwataka wasiegemee upande wa Tanzania kwa sababu nchi hiyo ina nia mbaya ya kuwagombanisha.

Taarifa hizo zinasema kwenye mawasiliano hayo ya siri, viongozi wa Rwanda walionyesha msimamo mkali wa kuitenga Tanzania na kuwaomba wabadili msimamo wao na wajiunge kwenye umoja wao.
"Rwanda iliilalamikia Burundi kwa nini imeungana na Tanzania, wakisema nchi hiyo inataka kuwatenganisha udugu wao wa damu, hivyo kuwaunga mkono ni kama kuwasaliti," kilisema chanzo hicho.
Hata hivyo, uongozi wa Burundi ulionyesha msimamo wa kutokubaliana na malalamiko hayo kwa kueleza wanachoamini nchi hizo tatu hazikufuata utaratibu wa EAC, kamwe haitakuwa tayari kuingia kwenye makosa hayo.

Akizungumzia suala hilo kwa njia ya simu kutoka Bujumbura, Waziri Nzeyimana alisema alichofanya ni kuondoa sintofahamu iliyokuwapo baada ya nchi hizo kuihusisha Burundi katika 'utatu' walioanzisha.

Alisema hakuna jambo la kuwasaliti lililofanyika, badala yake amewakumbusha nchi wanachama kufuata makubaliano na itifaki zilizowekwa katika kusimamisha jumuiya.

"Hatujawatosa (Rwanda) kama wanavyodai kilichofanywa na nchi hizo ni makosa makubwa na sisi kama nchi inayopenda sheria tunapinga na kuieleza dunia kwamba hatukushiriki na hatutashiriki katika umoja wao," alisema Nzeyimana.

Alisema katika vikao vilivyofanywa na nchi tano wanachama waliweka njia ya kufikia masuala mbalimbali ikiwamo Shirikisho la kisiasa, ambalo kwa sasa viongozi hao wamekubaliana kuanzisha kwa haraka.

"Tulikubaliana wote kwamba tuanze hatua kwa hatua hadi kufikia shirikisho, lakini tunasikia wenzetu wameanza na kuandaa rasimu ya katiba, hili ni jambo la kushangaza," aliongeza kusema.
Katika makubaliano hayo, nchi hizo zilikubaliana kuanza kushirikiana kwanza kwenye umoja wa soko la pamoja, umoja wa forodha, umoja wa fedha na sarafu na hatimaye kuja kwenye Shirikisho la kisiasa.

Hata hivyo, kwa mujibu wa Nzeyimana, bado hali haijatengemaa katika masuala hayo ya mwanzo, hivyo kuna haja ya kuimarishwa kabla ya kukimbilia kuwa na shirikisho moja la kisiasa.
Akizungumzia suala hilo, Naibu Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dk. Abdullah Juma Sadallah alisema bado anaunga mkono kauli ya Burundi kwa kuonyesha msimamo imara wa kuimarisha EAC.

Alisema kinachofanywa na nchi hizo ni kutaka kurudisha nyuma juhudi zilizochukuliwa na viongozi waliotangulia za kuziunganisha nchi hizo kwa maslahi ya wananchi wa kila nchi husika.
"Hatutaki kurudi kama huko nyuma, lakini ieleweke msimamo wa Burundi unataka kuimarisha jumuiya, tunawaunga mkono na wanaolalamika watakuwa na mambo mengine," alisema Dk. Sadallah.

Bado alisisitiza nchi hizo mbili hazitakubaliana na namna yoyote ya kutumia nguvu kuwashurutisha kukubaliana na mambo yaliyoundwa nje ya EAC.

CHANZO: NIPASHE JUMAPILI