Sunday 13 October 2013

Jumuiya ya vijana wa CUF yaionya UVCCM


13th October 2013

Jumuiya ya vijana ya Chama cha Wananchi (CUF) imetoa tamko kali kuhusu matusi na kejeli dhidi ya viongozi wao yanayotolewa na Jumuiya ya Vijana wa CCM (Uvccm).

Tamko hilo limetolewa na Makamo Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo, Yussuf Kaiza Makame, wakati akizungumza na waandishi wa habari katika ofisi za chama hicho Vuga mjini hapa.
Alisema kukaa kimya haina maana hawana la kusema au wanaogopa bali CUF kinaendeshwa kwa misingi ya maadili na kidemokrasia.


Alisema jumuiya hiyo imechoshwa na kauli za matusi zinazotolewa hasa kwa Katibu Mkuu wa chama hicho ambae ni Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad na sasa wamejipanga kikamilifu kokomesha vitendo hivyo kwa gharama yoyote.

Makamu mwenyekiti huyo alimtaka Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohammed Shein, kufahamu ana wajibu mkubwa wa kulinda amani ya nchi hivyo ameshindwa kukemea matusi yanayotolewa hadharani na CCM kwa kiongozi wao.

Alisema jumuiya ya vijana CUF inatambua kuwapo kwa kambi za makundi haramu ya vijana yalioandaliwa na CCM chini ya kiongozi mmoja wa serikali kwa lengo la kupiga kura zaidi ya mara moja katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015.

CHANZO: NIPASHE JUMAPILI