Thursday 24 October 2013

Tangu ujana wa Nyerere mpaka kupiga debe


Nyerere 

Mwaka 1945 kijana mmoja alikuwa anakaribia kuhitimu masomo yake katika chuo Kikuu cha Makerere huko Uganda akichukua shahada ya kwanza ya Elimu iliyomruhusu kuendelea na taaluma ya ualimu mara baada ya kutoka chuo katika mwaka huo huo. Lakini ilikuwa ni wakati huu akikadiriwa kuwa na umri wa miaka 23 alipoanza kuungana na wenzake wengine kuanzisha harakati za chini kwa chini. Hapana shaka kwa umri huo alikuwa ni kijana mdogo sana kiasi cha kuwa na ndoto nzito za kushiriki na wengine kuanzisha chama cha TAA (Tanganyika African Association) ili kiweze kuwa chachu na sehemu ya mapambano ya kuifanya nchi yake ya nyumbani kuwa huru kutoka katika ukoloni wa Mwingereza. Ilimchukua miaka kadhaa yeye na vijana wengine kuendelea na harakati ambazo baadaye zilizaa matunda.
Lakini ni wazi haikuwa rahisi sana. Najaribu kuelewa kuhusu ari ambayo alikuwa nayo yeye na wengine wakati huo, hasa ile dhamira ya kwamba kuna jambo moja kubwa linapaswa kufanyika tena kwa gharama hasa. Wengi wanajua haiwezekani mtu mmoja kufanya yote na kuwa shujaa kama walivyo mashujaa wa kwenye filamu ambao hawashindwi kitu. Historia inatueleza kuhusu wazee wengi wa maeneo tofauti walivyompokea kijana huyu mwenyeji wa Uzanaki na kumkaribisha miongoni mwao na kumpa msaada mkubwa ili kufikia yale malengo ya kuifanya Tanganyika kuwa huru.

Huyu ni Julius Kambarage Nyerere ambaye mwaka 1953 alichaguliwa kuwa raisi wa chama cha TAA ambapo mwaka mmoja baadaye walikigeuza na kuwa chama kamili cha siasa TANU (Tanganyika African Nation Union) chenye lengo la kutimiza azma ya kuifanya Tanganyika iliyokuwa chini ya utawala wa Waingereza wachache kuwa nchi huru yenye kutoa nafasi kwa watu wa rangi zote kufurahia uhuru na kujitawala. Baada ya mageuzi hayo TANU ikawa chama maarufu miongoni mwa wananchi wa wakati huo, kikipendwa na kukubalika na wengi.


Wakati mambo yakiendelea katika Umoja wa Mataifa mwaka 1954, suala kuhusu uhuru wa Tanganyika na namna wazalendo walivyokuwa wameamka katika kudai uhuru lilikuwa miongoni mwa ajenda ambazo zilizungumzwa. Jopo la wakaguzi kutoka UM likatumwa kuchunguza hali ya mambo na kujua utayari wa Tanganyika kuwa huru, lakini likiondoka na kushauri mpango wa miaka ishirini mpaka ishirini na tano kwa kulifanya taifa liwe huru. Kwamba Tanganyika haikuwa tayari. 

Bila shaka habari hizi hazikuwapendeza miongoni wa wote waliokuwa na kiu ya kujitawala. TANU wakapiga kura na kuamua kumtuma kijana wao Julius Nyerere kwenda kuhutubia katika baraza la UM kuelezea azma iliyokuwa inafukuta katika mioyo ya waTanganyika ya kutaka uhuru. Lakini kwa maombi ya serikali ya Uingereza basi Marekani ikaweka vikwazo kumzuia Nyerere kufanya kwa ukamilifu kile kilichompeleka UM ikiwemo kumtaka aondoke haraka mara tu baada ya kuhutubia hadhira ya Umoja wa Mataifa.

Haidhuru kama hayo yote yalitimia kwa matakwa yao lakini cha msingi kijana alifanya kazi yake na lililo kubwa zaidi ni kwamba uhuru ulipatikana licha ya mizengwe yote hiyo. Hii ilikuwa ni miaka kadhaa iliyopita ambayo ilijenga historia ya Tanganyika na baadaye Tanzania. Ilikuwa ni wakati ambapo vijana waliendesha serikali, waliendesha chama na kwa kiasi kikubwa walishika usukani katika nyanja nyingi.

Jambo linalonivutia kwa yakini ni vile ambavyo wazee wa wakati huo walipotumia hekima kubwa sana, lakini pia ujasiri wa kuweka matumaini yao kwa vijana. Wakiamini na kutoa msaada mkubwa ili vijana waweze kutimiza azma yao na kuikomboa nchi na pia kuindesha. Hili halikutokea tu Tanzania bali mahali pengi katika Afrika. Vuguvugu la ukombozi wa bara la Afrika lilishamiri sana na mapambano yalipata nguvu kwa kuwa vijana waliamka na walikuwa mstari wa mbele kuhakikisha kuwa jamii yao inakuwa huru. Kwa jasho na damu Afrika ilikombolewa, japo kwa uhuru wa bendera na kujitawala kwa kinadharia kama ambavyo tunaweza kushuhudia leo. Wapo walioishia ama kuteseka katika magereza ya wakoloni na watawala kama ilivyotokea kwa Nelson Mandela, Oliver Tambo, Walter Sisulu na wengineo ama waliouawa kabisa kama Steve Biko, Thomas Sankara, Patrice Lumumba na wengine. Haidhuru kama waliuawa kwa silaha yoyote ama risasi zilifyatuliwa kutoka katika viwambo vya bunduki zilizokuwa mikononi mwa weusi wenzao lakini inaeleweka kuwa kama si mapambano yao bila shaka, umauti usingewakuta katika hali hiyo.


Leo miaka kadhaa baada ya mapambano haya ya ukombozi, lakini vita bado haijaisha. Mapambano kwa vijana bado hayajaisha. Ukweli ni kuwa uhuru umepatikana kwa jasho na damu ambalo vijana walitoa na kwa msaada mkubwa wa hekima za wazee lakini mapambano yaliyobaki sasa ni ya kitabaka na kiu ya kutafuta usawa miongoni wa jamii zilizo huru za kiafrika. Inashangaza sana mara nyingine kuona ni kwa vipi hali ya mambo iligeuka na kufikia shime kwamba vijana ni taifa la kesho.


Lakini baadaye watu wakijikosoa kwa kubadili msemo pasipo kubadili muktadha mzima na kuanza kutia hamasa kwamba vijana ni taifa la leo. Leo ambayo haipo. Inastaajabisha sana kuona mustakabali wa vijana unavyokuwa na mashaka mengi. Nafasi ya vijana ni kama haipo ama haieleweki kabisa katika mchakato mzima wa ujenzi wa jamii iliyo na usawa na haki. Imezoeleka kwa namna ambavyo watu wamekuwa kwa vipindi tofauti wakikejeli vile ambavyo kwa kipindi kirefu ni majina ya watu wale wale yamekuwa yakijirudia katika duru za kiuongozi na kisiasa. 

Hata ilifika mahali ambapo imesemwa kuwa tangu kuzaliwa mpaka mtu anafikia umri wa utu uzima anaweza kubashiri nafasi ambayo mtu fulani anaweza kushika katika uongozi katika serikali nyingi za kiafrika na Tanzania hususani.


Hoja kuu ni kwamba vijana hawapo tayari ama hawajaiva ili kuweza kushika madaraka. Hii inashangaza sana kwa sababu ikiwa miaka ambayo mapambano ya uhuru yalishamiri, ilikuwa ni vijana waliosimama katika majukwaa ama katika maandamano ama ni Mau Mau waliotoka msituni kuendeleza harakati za kujikomboa. Inakuwaje leo hii vijana wanapotea kwa hoja ya kwamba wanahitaji muda kuweza kuiva na kuwa tayari. Lakini kukiwa hakuna mipango madhubuti ya kuwafanya vijana waweze kujijenga na kutambua nafasi yao katika jamii.


Ni rahisi sana kuonyesha upande mwingine wa vijana unaowaonyesha kama kizazi kisichokuwa na mwamko katika kujiendeleza na kuendeleza jamii yao, kwa sababu tu hatupo tayari kutambua jitihada mbalimbali zinazofanywa na makundi ya vijana ama kwa makusudi ama kwa kukosa dhamira. Katika jamii ambayo kiwango cha elimu kimeporomoka, ambapo hakuna mfumo unaoeleweka wa kuwaandaa vijana huwezi kutegemea kuwa na kizazi chenye kueleweka pia. Ikiwa kwa miaka kadhaa vijana wakipiga debe na kusisitiza umuhimu wa kuwa na baraza la vijana kama chombo kitakachowaunganisha kitaifa lakini madai hayo yakiwekwa kapuni, bado hatuoni dhamira ya kweli ya kuwafanya vijana waweze kutimiza azma yao hiyo.


Nyakati za sasa zimewagawa sana vijana katika makundi tofauti ya kiitikadi pasipo kuwa na mfumo mmoja wenye kueleweka wa kuwaendeleza na kutumia ipasavyo nguvukazi yao ili kusukuma mbele maendeleo ya taifa ama mataifa mengi ya kiafrika.

Ikiwa vijana ni sehemu kubwa ya jamii na bado sehemu hiyo kubwa inakosa nafasi ya kueleweka, jambo hili si ishara njema hata kidogo. Tulizowea kusikia kuwa ili kuendelea tunahitaji watu, siasa safi na uongozi bora. Sijui ni lipi kati ya haya matatu linatumika ipasavyo, ‘siasa safi, ‘uongozi bora’ na ‘watu.’ Watu hususani vijana, wako wapi leo hii ili kutufanya tuendelee ikiwa kwa nyakati zote tunapata kuwa na sura zilezile katika nyanja nyingi za kiuongozi. Hii ni kwa kuwa ‘hawapo tayari’ na pia ‘vijana wa sasa si kama wa zamani’ kwa sababu ‘vijana wa sasa wanaendekeza sana starehe kuliko kazi.’ Tumesikia sana kauli hizi. Ni kweli huwezi kufananisha vijana wa sasa na vijana wa zamani kwa sababu kadhaa. Mojawapo ni kuwa vijana wa zamani walipata kuungwa mkono sana na wazee ambao kwa makusudi waliweza kuwekeza kwa vijana wao ikiwemo kujenga misingi iliyo imara lakini pia wakijua kwamba vijana wanafahamu mengi na ni wepesi kukabili upinzani na mabadiliko ya kijamii. Hivyo hapa tunarudi nyuma na kutazama ni kwa kiasi gani vijana wa sasa wamejengewa misingi inayowawezesha kusimama na kutumia nafasi zao vizuri.


Wakati nilipokuwa mkoani Shinyanga jioni moja, tulikuwa watu wengi wapatao thelathini tumezunguka katika moto uliokuwa umekokwa na mzee mmoja wa kijiji. Moto huu unafahamika kama shikome, ama kikome maalum kwa kuwaweka vijana na wazee pamoja ili kujadili na kwa nyakati za zamani wazee kutoa maelekezo na maonyo kwa vijana. Lakini siku hiyo ni vijana waliomba moto huo kukokwa kwa kuwa kabla yake tulijadili sana kwanini mila hii ilipotea, bahati njema mzee mmoja aliridhia kuandaa tukio hilo hasa kwa kuwa vijana wengi hawakupata kulishuhudia zaidi ya kusikia tu habari zake.


Wakati wa maongezi wazee walielekeza sana lawama zao kwa vijana kwamba si wasikivu na wanakiuka misingi ya mila ambayo wao waliiheshimu na kwamba iliwakuza na kuwafanya kuwa wenye nidhamu. Lakini vijana walijibu kwa kuhoji ni nani anapaswa kulaumiwa ikiwa moto wa shikome ulizimwa na ilikuwaje wao hawakupata kuushuhudia mpaka walipoomba siku hiyo. Ni wazi kwamba wazee waliacha, hivyo vijana hawakuwa na uwezo wa kulinda mila ambayo iliharibiwa na wazee. Ilikuwa ni hoja ya msichana mmoja mdogo iliyohitimisha mjadala alipohoji, vijana wanaweza kufanya nini ama kupata wapi wasaa wa kuongea na wazee kama wazee hao wanatumia muda mwingi kujijali wenyewe, kukaa na kupiga soga kilabuni huku wakirejea usiku wakati watoto wameshalala.


Kwa namna hii pia, kizazi fulani kimeamua kulala kwa makusudi na kusahau kutoa nafasi kwa vijana kujiimarisha na kujifunza na zaidi kuchangia nguvu yao katika ujenzi wa jamii iliyo bora zaidi. Wanaobadili mitaala ya elimu si vijana. Hata baadaye tunaanza kubishana kama kweli kuna mitaala ama mihutasari tu  katika mfumo wetu wa elimu. Napata shaka kuamini kama ni vijana ndio wanashusha kiwango cha ufaulu ama kubinya fursa zilizopo katika jamii.

Kwa namna moja ama nyingine tunakumbatia ukoloni mamboleo na kuruhusu bila kuchuja mifumo mipya ya maisha ya utandawazi-wizi ambayo inaathiri mila zetu na kukiacha kizazi cha sasa bila kuwa na mwelekeo unaoeleweka. Si kwamba jamii ya vijana imeharibika kabisa, lakini tunapolaumu kuwa suruali zinashushwa chini ya makalio tunapaswa kuangalia ni nini tunachowaonyesha vijana katika runinga zetu katika kile tunachoita uhuru wa kupata habari. Uhuru wa kupata habari usio na mipaka katika kutambua athari za utandawazi na ukoloni mamboleo lakini kwa habari za maana ukiwa umejaa ukakasi ni jambo lisiloeleweka.
Sasa tunakuwa na kizazi cha vijana waliohitimu kupiga debe. Kutoka kizazi cha vijana waliokuwa mstari wa mbele katika kupigania ukombozi wa bara za Afrika mpaka kufikia kizazi cha vijana wanaoshinda vijiweni, bila shaka kuna mahali tumekosea, na mbaya zaidi tunaendelea kukosea, ama kwa bahati mbaya ama kwa kujua.
Na: Churchill Shakim
Churchill ni mwanaharakati wa masuala ya vijana na muziki wa asili ya HipHop.Anafanya kazi na shirika la TAMASHA.

*Mawazo katika makala hii ni yake binafsi na si msimamo au mtizamo wa shirika la TAMASHA.

imenakiliwa kutoka kwenye tovuti ya wewrite.or.tz