Thursday 24 October 2013

CAG Z’bar aiumbua ofisi ya Maalim Seif


Na  Mwinyi Sadallah , Mwananchi

Posted  Alhamisi,Oktoba24  2013  saa 24:0 AM
Kwa ufupi
 Ni katika matumizi mabaya ya fedha za umma kwa msimu wa Mwaka wa Fedha wa 2011/12.

Zanzibar. Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar, imekumbwa na kashfa ya kutuhumiwa kuwapo kwa matumizi mabaya ya fedha za umma kutokana na ripoti ya Mkaguzi Mkuu na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali ya mwaka 2011/12 visiwani hapa.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo ya ukaguzi wa hesabu kwa wizara, mashirika na taasisi za Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, jumla ya Sh295,977,000 zimelipwa kwa matumizi mbalimbali ya huduma kwa Makamu wa Kwanza wa Rais na mambo mengine bila ya kuwapo na vielelezo vya matumizi hayo.
Mkaguzi wa Hesabu za Serikali (CAG), Fatma Mohamed Said katika taarifa yake imesema, kukosekana kwa nyaraka za vielelezo vya matumizi ni kwenda kinyume na kanuni ya 95(4) ya kanuni za Fedha ya Mwaka 2005.
Alisema wakaguzi wa hesabu wameshindwa kupata uthibitisho wa malipo na matumizi ya fedha hizo na hivyo kushindwa, kujiridhisha kutokana na matumizi ya kiasi hicho cha fedha kama zilivyokuwa zimetoka kupitia hati, hundi na kiasi cha fedha kilichotumika.
CAG ameeleza kwenye ripoti hiyo kuwa, kati ya hundi zilizokosa nyaraka za matumizi yake, 12 zilitumika kufanya malipo, 8 zimehusu malipo aliyolipwa Makamu wa Kwanza wa Rais, Maalim Seif kwa viwango tofauti hadi Juni mwaka uliopita.
Wakati ufujaji huo ukitokea katika Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais, katika Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar, Balozi Seif Ali Idd nako kumekosekana kielelezo cha matumizi ya Sh10.5 milioni kupitia malipo yaliyofanyika Januari 24, mwaka jana.
Mbali na Ofisi ya Makamu wa Kwanza kushindwa kuwasilisha vielelezo vya matumizi ya fedha za walipakodi kiasi cha Sh19.575 milioni, vielelezo vya matumizi yake vimeshindwa kupatikana kwa maelezo kuwa fedha hizo zililipwa kampuni mbili ikiwamo ya Sami Trader na Queen Tour and Traveler kupitia hundi namba 392366 na 392494.
“Kukosekana kwa vielelezo ni kwenda kinyume na kanuni ya 95(4) ya kanuni ya fedha Zanzibar ya mwaka 2005 , kwa hali hiyo uhalali wa malipo hayo haukuweza kuthibitishwa,” alieleza CAG Fatma katika taarifa yake.
Mwananchi,Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar, Fatma Abdulhabib Ferej,alisema matumizi ya viongozi wakuu wa Serikali yanasimamiwa na Wizara ya Fedha kupitia mfuko maalumu wa Serikali.
‘Mimi sifahamu kama kuna matumizi yamekosa maelezo,wanaotoa fedha za huduma za viongozi ni Wizara ya Fedha,wao wanaweza kufahamu vizuri zaidi kwa sababu ndiyo wahusika wakuu,”alisema Fatma.
Kuhusu bajeti kupita kiwango kilichoidhinishwa na BLW alisema suala hilo ni geni kwake na hakumbuki Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais kuzidisha kiwango cha matumizi ya fedha licha ya suala hilo kuwa limeripotiwa katika ukurasa wa 92 wa ripoti ya mkaguzi mkuu wa Serikali Zanzibar.
Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha,Khamis Mussa alisema ni kweli ripoti ya CAG Zanzibar imehoji baadhi ya vielelezo na nyaraka lakini anaamini fedha zote zilizotoka zimetumika kama ilivyokuwa imekusudiwa.

Mussa alisema tatizo kubwa linalojitokeza ni kutokana na huduma za usafiri wa ndege za viongozi pale wanapolazimika kukodi na baadhi ya nyaraka kuchelewa kuwafikia zikiwamo nyaraka za malipo ya huduma(invoice) kutoka kampuni zinazohusika hivyo kuwapa wakati mgumu wanapofanyiwa ukaguzi.
Pia alisema watendaji dhamana bado wana nafasi ya kuwasilisha nyaraka za matumizi kwa CAG ili waweze kufuta taarifa zilizoripotiwa awali na kuonyesha kuwapo kwa matumizi ya fedha bila ya vielelzo na matumizi yake.
Hivi karibuni wajumbe wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar wamekuwa wakilalamika kuhusu vitendo vya ubadhirifu wa fedha za Serikali na kuundwa Tume mbalimbali za uchunguzi ikiwamo Baraza la Manispaa,Shirika la Umeme Zanzibar na ripoti kutoa mapendekezo ya wahusika kuwajibishwa na kuchukuliwa hatua za kisheria.

SOURCE: MWANANCHI