Thursday 17 October 2013

Ubabe wa Dk Magufuli unaumiza uchumi wa nchi


Posted  Alhamisi,Oktoba17  2013  saa 24:0 AM
Kwa ufupi
Kutokana na mvutano huo ni wazi kwamba usingekuwa na tija kwa Serikali wala Tatoa na Taboa, bali ungeleta maumivu makubwa kwa wananchi.

Tumeshuhudia mvutano kati ya Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli na Chama cha Wamiliki wa Malori Tanzania (Tatoa) ambao wanapinga sheria ya tozo ya asilimia tano kwa wasafirishaji wanaozidisha mizigo na kusababisha uharibifu wa barabara.

Mbali na Tatoa, Chama cha Wamiliki wa Mabasi Tanzania (Taboa) pia wanapinga sheria hiyo ya barabara namba 30 ya mwaka 1973 na marekebisho yake ya mwaka 2001.
Waziri Magufuli alisema anasimamia sheria hiyo ili kuhakikisha barabara haziharibiwi na watu wachache wenye nia ya kujinufaisha binafsi bila kujali masilahi ya Taifa.
Hata hivyo wamiliki hao kupitia Tatoa walisema Waziri huyo amerudisha tozo ya asilimia tano kwa maslahi yake na amekuwa mtu ambaye haambiliki, hashirikiani na wadau pamoja na kujichukulia sheria mkononi.
Wakizungumza hivi karibuni jijini Dar es Salaam wamiliki hao walieleza kuwa sheria hiyo iliyotangazwa na Magufuli ilianza kutumika Oktoba Mosi na kupatiwa barua Oktoba 2, mwaka huu ya kueleza kwamba tozo hiyo imeondolewa jambo ambalo lilisababisha msongamano. Hata hivyo Waziri Mkuu, Mizengo Pinga aliumaliza mgogoro huo na kuruhusu wamiliki wa magari hayo kuendelea na safari zao kwa mwezi mmoja wakati jitihada nyingine zikiendelea.
Pinda alisema kutokana na sakata hilo, amelazimika kuunda kamati ambayo itakutana na wadau, Tatoa na Taboa ili kupata ufumbuzi wa mgogoro uliojitokeza. Athari zilizojitokeza ni pamoja na kusimama kwa upakuaji na upakiaji wa mizigo katika Bandari ya Dar es Salaam, kukwama kwa usafirishaji wa mizigo ndani na nje ya nchi na kukwamisha biashara na huduma za jamii kwa wananchi.
Kutokana na mvutano huo ni wazi kwamba usingekuwa na tija kwa Serikali wala Tatoa na Taboa, bali ungeleta maumivu makubwa kwa wananchi.
Pamoja na ushupavu wake Dk Magufuli katika kusimamia sheria, mimi naona wakati mwingine atumie pia busara, kwani wakati mwingine sheria pekee hazitatui matatizo.
Ni kweli kwamba Dk Magufuli anasimamia sheria halali, lakini ajue kwamba sheria hizo hutungwa na Bunge linalowawakilisha wananchi. Dk Magufuli akitoa tamko lake anasema wasafirishaji wengi nchini ni wanasiasa, kama wanaona kuondolewa kwa ofa ya uzito uliozidi wa asalimia tano wapeleke hoja bungeni ipitishwe rasmi.
Dk Magufuli akaendelea kusema kuwa, wanaogomea ni matajiri hivyo waende mahakamani.
Ubabe huu hauna tija yoyote, badala yake anashiriki kwa namna moja au nyingine kuhujumu uchumi wa nchi.
Nchi yetu inapaswa kuondoa vikwazo hivyo ili kuimarisha biashara za ndani na nje ya mipaka yake. Nchi yetu hii ina bandari ambayo inategemewa na nchi kama vile Zambia, Zimbabwe, Rwanda, Burundi, Malawi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC). Anachotakiwa kufanya Dk Magufuli ni kuimarisha utengenezaji wa barabara kwa kuongeza kiwango cha ubora ili magari yachukue uzito mkubwa zaidi.

Kwa upande mwingine, Serikali ichukue changamoto hii kama nafasi ya kufufua Mashirika ya Reli ya TRC na Tazara badala ya kuachia tu malori yasafirishe mizigo. Wakati sasa umefika mizigo isafirishwe kwa reli ili kuepuka msongamano wa magari, uharibifu wa barabara na kuharakisha mizigo inafika kwa wateja kwa wakati.
Kazi ya Waziri Mkuu Pinda isiwe kusubiri migogoro tu, bali aisimamie Serikali ifufue njia mbadala za usafiri. Ni aibu kwa nchi yetu yenye zaidi ya miaka 50 ya uhuru, inashindwa kuendesha mashirika ya usafirishaji kwa mfano shirika la reli na ndege ambayo yaliyoachwa na wakoloni.
0754 897 287