Monday 26 August 2013

Waislamu wasisitiza Mahakama ya Kadhi

Wajumbe wa Baraza la Katiba kutoka Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania wakipitia vifungu mbalimbali vya Rasimu ya Katiba Mpya Dar es Salaam, jana. Picha na Venance Nestory 

Na Raymond Kaminyoge, Mwananchi  (email the author)

Posted  Jumatatu,Agosti26  2013  saa 9:55 AM
Kwa ufupi
Alisema Waislamu wengi waliotoa maoni yao kwenye Tume ya Mabadiliko ya Katiba, walitaka kuwapo kwa mahakama hiyo lakini cha kushangaza tume hiyo iliyatupa.


Dar es Salaam. Wajumbe wa Baraza la Katiba la Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania, wametaka kipengele cha Mahakama ya Kadhi kiwekwe kwenye Katiba Mpya.
Amiri Mkuu wa Baraza Kuu la Jumuiya na Taasisi za Kiislam, Sheikh Mussa Kundecha, alisema jana kuwa ingawa rasimu ya Katiba haina kupengele hicho, lakini wao wanaona hiyo ni haki yao.
“Tunataka kipengele cha Mahakama ya Kadhi kiwekwe Katiba Mpya na  iendeshwe na kugharamiwa na Serikali,” alisema Sheikh Kundecha wakati wajumbe hao walipokuwa wakijadili rasimu ya Katiba.
Alisema Waislamu wengi waliotoa maoni yao kwenye Tume ya Mabadiliko ya Katiba, walitaka kuwapo kwa mahakama hiyo lakini cha kushangaza tume hiyo iliyatupa.
“Sasa licha ya kwamba kipengele hicho hakipo kwenye rasimu, bado tunaendelea na kilio chetu cha kutaka kiwekwe,” alisema.
Hata hivyo, Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba, wiki iliyopita alisema kipengele ambacho hakipo kwenye rasimu hakitawekwa kwenye Katiba Mpya.
Sheikh Kundecha alihoji iweje kuwe na Mahakama za Biashara inazoendeshwa na Serikali, wakati kuna Watanzania wachache ambao ni wafanyabiashara.
“Kuna wafanyabiashara wachache lakini wana mahakama yao, kunakuwa na ugumu gani kuweka Mahakama ya Kadhi  kwa ajili ya Waislamu?” alihoji Kundecha. Mwaka jana, Serikali iliruhusu kuanzishwa kwa Mahakama ya Kadhi ambayo iko nje ya mfumo  wa Serikali.

source: Mwananchi news paper