Friday 1 November 2013

Polisi mbaroni kwa kupora Sh220 mil


Na Daniel Mjema,Mwananchi

Posted  Ijumaa,Novemba1  2013  saa 24:0 AM
Kwa ufupi
Wadaiwa kuwa wamesharejesha Sh80 milioni baada ya kubanwa na makachero wa polisi.


Moshi. Askari polisi wawili wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU), wametiwa mbaroni kwa tuhuma za kula njama na kushiriki katika uporaji wa Sh220 milioni za Kampuni ya Dot Services ya mjini Moshi.

Habari za uhakika zilisema baada ya kubanwa na makachero, askari hao walirejesha Sh60 milioni na watuhumiwa wengine wawili ambao ni raia, walirejesha Sh23 milioni. Askari hao ni wale walioko katika Kikosi cha Polisi wa doria wanaotumia pikipiki na jana watuhumiwa wote walitawanywa katika vituo mbalimbali ili wahojiwe kwa nyakati tofauti tofauti.
Habari za kipolisi zilisema askari hao hawakwenda eneo la tukio lakini walifahamu mpango mzima kuhusu uporaji huo uliowawezesha kupata mgawo wa fedha hizo.
Waliotiwa mbaroni wana vyeo vya Constable (majina tunayo) na inaelezwa kuwa tukio hilo limewachukiza baadhi ya polisi wakidai ni kuwa mfululizo wa matukio yanayochafua sura ya jeshi hilo.
Habari hizo zimebainisha kuwa tukio hilo ni mpango mahususi uliowashirikisha watu wasiopungua 10 wakiwamo baadhi ya watumishi wa Kampuni ya Dot Services waliovujisha mpango wa kuhamisha fedha hizo.
Kulingana na vyanzo vya habari, idadi ya walioshiriki katika mpango wa kupora fedha hizo ni kati ya watu wanane na 10 na tayari polisi wameanzisha msako mkali wa kuwatafuta.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa Kilimanjaro, Robert Boaz alikaririwa akisema kuwa fedha hizo ziliporwa Jumanne asubuhi katika makutano ya Barabara za Arusha na Boma mjini Moshi.
Kwa mujibu wa Kamanda Boaz, baada ya kufika katika makutano hayo, wafanyakazi wa Kampuni ya Dot Services waliokuwa na gari aina ya Toyota Hilux T.864 AZM walisimama kuruhusu pikipiki ipite.
Kamanda Boaz alisema wakati wakisubiri pikipiki ipite, ghafla walijitokeza watu wawili wakafungua milango na kuingia ndani ya gari na kuwateka wafanyakazi na kuwaamuru waelekee eneo la Shanty Town.
Hata hivyo mkurugenzi wa Fedha wa kampuni hiyo ya ujenzi yenye makao yake makuu nchini Uganda, Shuresh Bab alifanikiwa kuruka kwenye gari hilo na kutoa taarifa polisi.
Kamanda Boaz alifafanua kuwa msako wa kuwatafuta wahusika ulianza mara moja ambapo polisi walifanikiwa kulipata gari hilo na wafanyakazi wakiwa wametelekezwa mto Karanga mjini Moshi.
 
SOURCE: MWANANCHI