Tido Mhando 
            
Posted Jumapili,Agosti18 2013 saa 13:26 PM
Kwa ufupi
Tido Mhando amefanya kazi ya utangazaji wa redio kwa
 muda mrefu sana.  Aliifanya kazi hii hapa Tanzania, Kenya na Uingereza,
 ikampatia umaarufu mwingi.
Tido Mhando amefanya kazi ya utangazaji wa redio
 kwa muda mrefu sana.  Aliifanya kazi hii hapa Tanzania, Kenya na 
Uingereza, ikampatia umaarufu mwingi. Je, maisha kama mtangazaji wa aina
 yake yalikuwaje katika enzi hizo? Tido analijibu swali hili katika 
simulizi zake hizi za kila Jumapili. Wiki iliyopita alitufahamisha 
mwanzo wa kuwika kwa mwanariadha ambaye, labda, ni bora kuliko wote 
Tanzania hadi sasa, Filbert Bayi, pale alipomshinda mkongwe wa riadha wa
 Kenya, Kipchoge Keino mwaka 1973. SASA ENDELEA...
Naweza kusema bila ya tashwishi yoyote kwamba, 
mwaka huo wa 1973 ndiyo uliokuwa  mwaka wangu wa mabadiliko makubwa sana
 kazini na hata katika hali ya maisha yangu binafsi.
 Kama nilivyoeleza hapo nyuma, huo ulikuwa ni 
mwaka ambao niliteuliwa, kwa mara ya kwanza, kwenda kufanya kazi nje ya 
Tanzania, pale nilipotumwa nchini Uganda kutangaza mashindano ya mpira 
ya nchi za Afrika Mashariki.
 Baada ya Filbert Bayi kumshinda Kipchoge Keino 
kule Lagos Nigeria, mwaka huo huo wa 1973, taifa la Tanzania likawa 
limeingiwa na msisimko mkubwa sana kuhusiana na michezo hii ya riadha na
 hasa ile ya kimataifa.
 Watanzania, hasa vijana, wakaanza kuchakarika 
kwelikweli na kujiingiza kwa wingi kwenye fani hii, huku Serikali nayo 
ikionyesha nia ya dhati ya kutaka kuiendeleza katika ngazi zote.
 Sisi pia pale Radio Tanzania Dar es Salaam (RTD),
 kila ilipowezekana tulifuatilia kwa karibu maendeleo hayo kwa kutangaza
 sana habari za mashindano mbalimbali ya riadha, iwe ya shule za msingi,
 sekondari na vyuo, hasa yale ya kitaifa na kimataifa.
 Kwa jumla ilipofika wakati huu, tayari nilikuwa 
najitambua kama miongoni mwa watangazaji walioanza kushamiri; nyota 
yangu ilikuwa imeanza kupata nuru yake.
 Nakumbuka siku moja katika mwaka huohuo wa 1973, 
tukiwa tunakaribia mwishoni mwa mwaka, aliyekuwa Mkurugenzi siku hizo, 
Paul Sozigwa, aliita mkutano adimu wa watangazaji wote.
 Nasema ulikuwa mkutano adimu kwani si mara nyingi
 mkuu huyo alikuwa anakutana nasi hivi, kwa hiyo tukajua bila ya shaka 
kuna mambo makubwa ambayo alitaka kutufahamisha au kushauriana nasi.
 Ikumbukwe ya kwamba hili lilikuja muda mfupi tu 
baada ya mimi kurejea kutoka Uganda, Uganda kwa Idi Amin Dada, Idi Amin 
ambaye tayari alikuwa ameshaanza kuzusha chokochoko na Tanzania.
 Halafu mkuu wetu huyo, Sozigwa, hakuwa tu mkuu wa
 kawaida. Alikuwa mtu mwenye kauli ya kutambulika na utawala wa ngazi za
 juu. Alikuwa karibu sana na Rais Mwalimu Julius Nyerere.
Sozigwa alikuwa mtu wa kuzingatia maadili sana, kwa hiyo aliaminika pia kwa kiasi kikubwa katika chama tawala siku hizo, chama pekee cha siasa huku Tanzania Bara, chama cha Tanu. Ikumbukwe kule visiwani kulikuwa na chama cha Afro Shirazi. Kwa jumla chama cha Tanu kilimtumia sana mkurugenzi huyu kwenye mambo yake ya propaganda zake. Kwa kweli alikuwa na uwezo wa hali wa juu kwenye eneo hilo.
Sozigwa alikuwa mtu wa kuzingatia maadili sana, kwa hiyo aliaminika pia kwa kiasi kikubwa katika chama tawala siku hizo, chama pekee cha siasa huku Tanzania Bara, chama cha Tanu. Ikumbukwe kule visiwani kulikuwa na chama cha Afro Shirazi. Kwa jumla chama cha Tanu kilimtumia sana mkurugenzi huyu kwenye mambo yake ya propaganda zake. Kwa kweli alikuwa na uwezo wa hali wa juu kwenye eneo hilo.
 Kwani ni yeye Sozigwa  ndiye aliyekuwa mtu wa 
mwanzo kabisa kuandika yale yaliyokuja kutokea kuwa labda mazungumzo 
bora ya habari kuwahi kutangazwa na redio yoyote barani Afrika.
 “Mazungumzo Baada ya Habari” yalikuwa na kila 
kitu ambacho msikilizaji alikihitaji na yeye mwenyewe kulengwa. 
Yaliandikwa kwa ufasaha mkubwa. Yaliandikwa kwa lugha yenye mvuto 
sikioni na yalisomwa kwa umakini wa hali ya juu na wasomaji bora wenye 
sauti adimu zenye mvuto.  Yalikuwa ni mazungumzo yaliyobeba ujumbe mzito
 wa kitaifa kwa watu wote, ujumbe uliotakiwa kueleweka na kila mtu bila 
ya taabu yoyote. Dhamana hii kwa mara ya kwanza aliibeba Sozigwa na 
kuitekeleza kwa ufanisi usio na kifani.
 Kila siku iendayo kwa Mungu, mara tu baada ya 
taarifa ya habari ya saa 2:00 usiku, Watanzania kwa mamilioni walikuwa 
wakitega sikio kusikiliza kipindi hiki cha dakika chache tu cha 
“Mazungumzo Baada ya Habari.” 
Zilikuwa dakika chache za kusisimua. Dakika chache
 zilizojaa kipaji cha  ubunifu wa kiwango kikubwa cha kumakinika. Dakika
 chache ambazo msikilizaji alikuwa anaelimika, anaburudika na pia 
anafahamishwa.  Mara zote, mazungumzo haya yalikuwa yakianza kwa hadithi
 ya aina fulani. Mara nyingi, mwandishi Sozigwa akizibainisha humo kuwa 
ni ya hadithi ya kweli.  Kama ni kweli, bali mwandishi huyu alikuwa 
akifahamu mengi, tena mengi mno!
 Nazikumbuka sana hadi leo baadhi ya hadithi 
nyingi hizi za kusisimua. Ikiwa ni pamoja na ile ya “Uchu wa Mzee 
Mikidadi”, iliyohusu mwanafunzi mmoja kutoka Shule ya Sekondari ya 
Mpwapwa ambaye wakati mmoja wa likizo alimkaribisha rafiki yake waende 
naye nyumbani kwao.
 Kama ilivyo kawaida, walipofika nyumbani kwa Mzee
 Mikidadi, walikaribishwa vizuri sana. Baba akaamuru lichinjwe jogoo 
kubwa kuliko yote miongoni mwa kuku wake ili mwanaye na mgeni wake 
waweze kufurahi.
 Ilipofika wakati wa chakula, Mzee Mikidadi na 
vijana wake wawili wakaketi pamoja kufaidi mlo wao huo huku mzee 
mwenyewe akichukua madaraka ya kugawa kile kitoweo  akisema “Kuleni 
wanangu, leo siku kuu yenu!”
  Wakati akisema hayo  mwenyewe alikuwa 
akijichukulia yale mapaja ya kuku makubwa yaliyonona pamoja na vitamu 
vinginevyo kama vile firigisi na kuwaachia wale vijana vipapatio.
 Hatimaye mazungumzo yale yalikuwa yakihitimishwa 
na ujumbe mzito kwa wote, ujumbe uliokuwa ukifikia kila mtu, wake kwa 
waume, wazee, vijana na hata watoto. Wafanyakazi na wakulima na hata 
wasiokuwa na kazi. Wasomi na wasiosoma. Kila mtu aliyapenda na 
kuyafuatilia kwa umakini wa hali ya juu.  
Kwa ujumla Watanzania wote waliyapenda mazungumzo 
yale ya habari. Ulikuwa ni wakati rasmi wa kufahamu msimamo wa chama na 
serikali kuhusu jambo fulani. Liwe la kisiasa au la kijamii. Liwe la 
kitaifa au la kimataifa, Sozigwa alikuwa anatufahamisha msimamo halisi.
 Lakini hitimisho wa ujumbe huu, lilikuwa ni ule 
usomaji wake wa kipekee. Walikuwa mara kwa mara wakitumiwa wasomaji 
wenye sauti adimu za mamlaka zenye uwezo wa kuwasilisha ujumbe muhimu 
kama huu.
Kwa maana hii, na hasa katika siku zile za mwanzoni kabisa, wasomaji wa kipindi hiki walichaguliwa kwa umakini mkubwa. Hakuwa kila mtu tu anachaguliwa kusoma hata kama ulikuwa msomaji mzuri namna gani.
Kwa maana hii, na hasa katika siku zile za mwanzoni kabisa, wasomaji wa kipindi hiki walichaguliwa kwa umakini mkubwa. Hakuwa kila mtu tu anachaguliwa kusoma hata kama ulikuwa msomaji mzuri namna gani.
 Walikuwepo wachache tu waliokuwa na sauti za 
uzito huu, sauti zilizokubalika kwa mvuto wa aina yake. Nawakumbuka 
wachache wao wa mwanzoni siku zile. Wa kwanza alikuwa Abdul Baker halafu
 pia alikuwepo Abdul Ngarawa na baadaye akaja Juma Ngondae. Wakitakiwa 
kuwasilisha kwa umakini ubunifu huo wa Paul Sozigwa. 
Huyo basi ndiye aliyekuwa mkurugenzi wetu hapo RTD
 katika mwaka huo wa 1973. Ndiye aliyekuwa ametuita watangazaji wote 
kwenye mkutano wa aina yake siku hiyo isiyokuwa na jina katika jambo 
ambalo kamwe hatukulijua.
 Tulikusanyika mapema kama tulivyotakiwa sote 
kwenye ofisi kubwa ya iliyokuwa idara ya idhaa ya taifa, tukimsubiri 
mkurugenzi. Mimi nilikuwa bado na stori zangu za Uganda, nikiendelea 
kuzimwaga kila nilipopata nafasi.
 Kwa hiyo katika siku hii, nilikwenda kuketi nyuma
 kabisa na baadhi ya wale niliokuwa nimezoeana nao zaidi na kuanza kutia
 stori zangu hizo. Wala sikustuka sana wakati mkurugenzi alipoingia na 
kuanza kuzungumza, kwani bado kwa kiasi fulani mimi niliendelea 
kunong’ona. 
Kwa jumla alizungumza kwa kirefu kuhusu hali ya 
kisiasa ilivyokuwa nchini wakati ule na wajibu wetu kama shirika la 
Serikali. Kwa kiasi, alidokeza kuhusu tishio la Idi Amin Dada na pia 
akatupongeza mimi na Mshindo Mkeyenge kwa kazi nzuri tuliyokuwa 
tumeifanya kule Uganda.
 Nikiri ya kwamba bado tu sikuwa msikivu hivyo wa 
yale aliyokuwa akiyazungumza. Kumbe ghafla, mkurugenzi alibadili 
mazungumzo na kufahamisha ya kwamba menejimenti ilikuwa imeamua kuwa kwa
 mara ya kwanza kabisa katika historia ya RTD, itatuma watangazaji 
kufuatana na timu ya wanamichezo wa Tanzania watakaoshiriki kwenye 
michezo mikubwa ya Jumuiya ya Madola huko Christchurch, New Zealand, 
mapema mwaka unaofuata wa 1974.
 Mkurugenzi akaendelea kusema kwamba uamuzi huo 
ulizingatia umaarufu wa Tanzania hasa kwenye michezo ya riadha kufuatia 
kukua kwa umahiri wa mwanariadha Filbert Bayi.
 Pamoja na yote hayo mimi kule nyuma ya chumba cha
 mkutano bado nilikuwa naendelea na porojo zangu kiasi ya kwamba 
sikuweza kumsikia  mkurugenzi aliposema ya kwamba pia menejimenti 
imewachagua wale inayoamini wanao uwezo mkubwa wa kuifanya kazi hiyo kwa
 ubora unaotakiwa.
 Kwa mstuko wa wengi kwenye mkutano ule, Sozigwa 
akalitaja jina la Tido Dunstan Mhando na mwenzangu Abdul Omar Masoud 
kwamba ndio tulioteuliwa kwa safari hiyo. 
Kwa sababu ambazo sikuzifahamu, Abdul Masoud 
hakuwepo kwenye mkutano huo, halafu nami sikuwa msikivu wa dhati, kwa 
hiyo hata sikuwa nimemsikia mkurugenzi alipolitamka jina langu. 
Na kwa kweli ingawaje kwa kiasi nilikuwa 
nimemsikia alipoanza kuelezea kuhusu uamuzi huo wa kupeleka watangazaji 
kwenye msafara huo utakaokwenda New Zealand, lakini kamwe, tena niseme 
kamwe, sikuwa na fikira zozote ya kwamba ingewezekana nikawa mmojawapo.
Hasa kwa kuwa ilikuwa imekwishazoeleka kuwa safari kama hizi zilikuwa zikipewa watangazaji waandamizi; mimi sikuwa miongoni mwao. Kwa hiyo, nilishangaa kuona ghafla macho ya watangazaji wenzangu wote waliokuwemo ndani ya mkutano ule yakinigeukia mimi!
Hasa kwa kuwa ilikuwa imekwishazoeleka kuwa safari kama hizi zilikuwa zikipewa watangazaji waandamizi; mimi sikuwa miongoni mwao. Kwa hiyo, nilishangaa kuona ghafla macho ya watangazaji wenzangu wote waliokuwemo ndani ya mkutano ule yakinigeukia mimi!
ITAENDELEA JUMAPILI IJAYO…
Mwananchi news paper
Mwananchi news paper
 
  