Thursday 18 July 2013

Maofisa wa Wizara ya Fedha kizimbani

            

 
Na James Magai,Hadija Jumanne  (email the author)

Posted  Jumatano,Julai17  2013  saa 21:31 PM
Kwa ufupi
Wanakabiliwa na mashtaka ya ufisadi wa mamilioni ya fedha za matangazo kwenye vyombo vya habari, wengine wawili wasakwa


Dar es Salaam. Maofisa wawili wa Wizara ya Fedha wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi. Wanatuhumiwa kwa ufisadi wa fedha za utoaji wa matangazo na habari kwa vyombo mbalimbali vya habari.
Maofisa waliopandishwa kizimbani ni pamoja na Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Ununuzi, Ernest Simon Mwakitalu na Ofisa Ununuzi, Liipu Neligwa ambao walisomewa mashtaka na Mwendesha Mashtaka wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Leonard Swai.
Wakati maofisa hao wawili wakipandishwa kizimbani na kusomewa mashtaka hayo, wengine wawili ambao walitakiwa kupandishwa kizimbani, Mkuu wa Kitengo cha Habari, Ingiahedi Mduma na Mkurugenzi wa Kampuni ya And- Line (2000) International, Daniel Ukwaya hawakuwapo mahakamani hivyo, mashtaka dhidi yao hayakusomwa hadi watakapokamatwa.
Washtakiwa hao wote kwa pamoja wanakabiliwa na jumla ya mashtaka 19. Shtaka moja ni kula njama kutenda kosa, mashtaka manane ya kutumia nyaraka za uongo ili kumdanganya mwajiri.
Mengine ni shtaka moja la matumizi mabaya ya madaraka, mashtaka manane ya kughushi, shtaka moja la ubadhirifu na shtaka moja la kusababisha hasara ya Sh19.8 milioni, ambalo ni shtaka mbadala kwa wote.
Akisoma hati ya mashtaka, Wakili Swai alisema washtakiwa hao walitenda makosa hayo kwa tarehe tofauti kati ya Juni na Julai, 2009.
Wakili Swai alidai kuwa washtakiwa hao walisaini hati za ununuzi zenye taarifa za uongo kwa lengo la kuonyesha kuwa Kampuni ya And Line (2000) International ilipewa fedha kwa ajili ya vipindi vinane vya matangazo katika vyombo vya habari vya redio, magazeti na runinga.
Alidai kuwa taarifa hizo kwenye vyombo vya habari zilihusu maonyesho ya 33 ya Biashara ya Kimataifa yaliyofanyika Dar es Salaam katika Viwanja vya Mwalimu Nyerere, Kilwa Road, kuanzia Juni 28 hadi Julai 10, 2009, kwa thamani ya Sh19.8 milioni, jambo ambalo si kweli.
Baada ya kuwasomea mashtaka, Wakili Swai alisema upelelezi wa kesi hiyo umekamilika na kuiomba Mahakama ipange tarehe nyingine ya kutajwa ambayo washtakiwe wengine watakuwa wamekamatwa ili wasomewe maelezo ya awali kwa pamoja.
Washtakiwa waliokuwapo mahakamani jana walikana tuhuma dhidi yao na waliachiwa huru kwa dhamana baada ya kutimiza masharti ya kila mmoja kusaini hati ya dhamana ya Sh5 milioni, kuwa na wadhamini wawili wanaotambulika, ambao pia walisaini hati ya dhamana ya kiasi hichohicho.
Kesi hiyo iliahirishwa na Hakimu Mkazi, Nyigulile Mwaseba hadi Agosti 15, mwaka huu itakapotajwa tena.