Friday 12 July 2013

Wilfred Lwakatare alazwa Muhimbili


                        
Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama wa Chadema, Wilfred Lwakatare akiwa amelazwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Dar es Salaam, jana, kutokana na kusumbuliwa na maradhi ya Shingo. 

Na Aziza Masoud, Mwananchi  (email the author)

Posted  Alhamisi,Julai11  2013  saa 15:4 PM
Kwa ufupi
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi kwenye wodi ya uchunguzi ya Sewahaji, Lwakatare alisema kuwa anakabiliwa na matatizo ya pingili za shingo na jopo la madaktari linakutana leo kuamua kama afanyiwe upasuaji ama la.

Dar es Salaam. Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Wilfred Lwakatare amelazwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili kutokana na matatizo ya shingo.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi kwenye wodi ya uchunguzi ya Sewahaji, Lwakatare alisema kuwa anakabiliwa na matatizo ya pingili za shingo na jopo la madaktari linakutana leo kuamua kama afanyiwe upasuaji ama la.
“Nilifanyiwa uchunguzi kwa x-ray na madaktari walisema hakuna jinsi zaidi ya upasuaji na kesho (leo) jopo la madaktari linasoma picha za x-ray kuamua aina ya upasuaji...nimegundulika kuharibika pingili ya sita na saba.
“Nilipata ajali mwaka 2008 na nilipona, lakini nilipatwa na kadhia hii baada ya kufikishwa Kituo Kikuu cha Polisi baada ya kukamatwa na zaidi ni kutokana na kulala chini,” alisema Lwakatare akiwa kitandani.
Alisema kuwa aliwahi kuumwa akiwa Gereza la Segerea alikokuwa anashikiliwa kabla ya kuachiwa kwa dhamana na kwamba alihudumiwa.
Alisema tatizo hilo lilijirudia jana asubuhi ambapo alifikishwa hospitali hiyo na kupatiwa kitanda kabla ya kufanyiwa vipimo vya X-ray na kukutwa tatizo hilo ambalo alisema gharama yake ni Sh3.5 milioni.