Rais wa Tanzania, Jakaya KIkwete 
            
Kwa ufupi
Ingawa Kikwete hakuitaja Chadema kwa jina, lakini 
chama hicho ndicho pekee kilichosusia kongamano la kutafakari amani 
kikidai kwamba Serikali haitendi haki.
Dar es Salaam. Rais Jakaya Kikwete (pichani) 
amekiponda Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kwa kuanzisha 
kikundi cha mgambo akisema hatua hiyo imejidhihirisha kwamba chama hicho
 hakipendi amani.
Ingawa Kikwete hakuitaja Chadema kwa jina, lakini 
chama hicho ndicho pekee kilichosusia kongamano la kutafakari amani 
kikidai kwamba Serikali haitendi haki.
Kikwete alisema hayo jana wakati akifunga kongamano hilo lililoandaliwa na Kituo cha Demokrasia Tanzania (TCD).
Chadema ilisusia kongamano hilo ikisema kuwa amani haitafutwi kwa kufanya makongamano kama ilivyofanya TCD.
“Chama cha siasa kuanzisha kikundi cha wanamgambo 
kwa ajili ya kupiga watu ni kiashiria kwamba chama hicho hakitaki amani 
bali kinaridhishwa na vurugu,” alisema Kikwete na kuongeza kuwa 
wanaopenda amani humaliza tofauti zao kwa kuzungumza.
“Tusiiache nchi yetu ije kulindwa na majeshi ya 
Umoja wa Mataifa, tusije kufikia huko, tujitahidi kuondoa tofauti zetu 
kwa njia ya mazungumzo,” alisema Kikwete.
Juzi Chadema walitangaza kwamba wataanzisha 
mafunzo kwa vijana wao kwa ajili ya kuwalinda ikidai kuwa dola imekuwa 
haisikilizi madai yao.
Alisema wanaosusa kongamano hilo wangeweza kufika 
wangeweza kutoa madukuduku yao kwa sababu viongozi wa Serikali na polisi
 walikuwapo lakini bado hawataki.
“Sasa hawa kweli wanapenda amani yetu wakati 
hawapendi kuja tuzungumze, wanataka watu wauane ama wapigane,” alisema 
kwa mshangao Kikwete.
Alisema Serikali na viongozi wake hawapendi vurugu
 na kwamba chama hicho kinafanya vurugu hizo ili kuwatoa katika ajenda 
za kuwaletea maendeleo Watanzania.
Hata hivyo aliwapongeza Chadema kwa kushiriki katika maandalizi ya kongamano hilo licha ya kususia kushiriki.
 
  