 
  
            
Duka moja wapo la Home Shopping Centre lililopo jijini Dar es Salaam 
            
Kwa ufupi
Mfanyabiashara maarufu jijini Dar es Salaam ameshambuliwa kwa kumwagiwa tindikali
Dar es Salaam. Mtu asiyejulikana juzi usiku alimvamia mmiliki wa maduka ya Home Shopping Centre, Said Mohammed Saad (pichani) na kumwagia maji usoni yanayodhaniwa kuwa ni tindikali.
Tukio hilo lililotokea juzi saa 1 usiku karibu na 
kituo cha Polisi cha Oysterbay, lilithibitishwa na Kaimu Kamanda wa 
Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Ally Mlege kwa kusema kuwa bado 
polisi wanaendelea na uchunguzi wao ili kuwabaini waliohusika.
“Ni kweli tukio hili limetokea ila polisi 
wanaendelea na uchunguzi. Tukikamilisha uchunguzi tunatarajia kutoa 
taarifa kamili za tukio zima,” alisema na kuongeza;
“Hatuna haja ya kuficha ukweli wa tukio hili, uchunguzi wetu ukikamilika na watuhumiwa wakikamatwa kila mtu atajua.”
Taarifa za uhakika kutoka ndani ya Jeshi la Polisi
 zilizolifikia gazeti hili zilieleza kuwa mtu huyo, alimkuta Saad akiwa 
anazungumza na mmoja wa wafanyakazi wake katika duka lake jipya lililopo
 karibu na Kituo cha Polisi cha Oysterbay.
“Wakati akizungumza na mfanyakazi wake, huyo mtu 
alikuwa kama anapita na alichomoa kitu fulani na kummwagia Saad usoni na
 kisha kukimbia,” zilieleza taarifa hizo na kuongeza;
“Baada ya tukio hilo alipelekwa katika Hospitali 
ya AMI, sasa hatujui kama bado yupo hapo au ameondoka, ila sisi 
tulizungumza naye na alitueleza mwonekano wa mtu aliyemwagia tindikali.”
Taarifa hizo zilifafanua kwamba polisi wanazitumia taarifa hizo walizopewa na Saad, ili kuweza kumkamata mhusika.
Taarifa hizo zilifafanua kuwa polisi wanapanga 
tena siku ya kumhoji kwa mara ya pili Saad, kwamba watataka kufahamu 
kama mfanyabiashara huyo alikuwa akipewa vitisho au ujumbe wowote, kabla
 ya kukutwa na tukio hilo.
Hata hivyo, habari nyingine zilizolifikia 
Mwananchi Jumapili zilieleza kuwa mtu huyo baada ya kummwagia Saad 
tindikali, alipanda pikipiki na kutokomea eneo hilo.
“Walikuwa wawili, mmoja alikwenda kufanya unyama 
na mwingine alibakia katika pikipiki, baada tu ya kumwagia tindikali mtu
 yule alikimbia mpaka pale alipokuwa imesimama pikipiki, alipanda na 
kuondoka kwa kasi,” zilieleza habari hizo.
Taarifa zilizopatikana jana asubuhi zilieleza kuwa
 ndugu na marafiki wa mfanyabiashara huyo, walikuwa katika mipango ya 
kumpeleka nje ya nchi kwa ajili ya kupatiwa matibabu zaidi.
Source. Mwananchi news paper
Source. Mwananchi news paper
