“Huwezi kutenganisha rushwa kubwa na dawa za kulevya, hawa wasichana 
wetu waliokamatwa Afrika Kusini , lazima kuna mtu mkubwa aliye nyuma 
yao,siyo wao,”
Reginald Mengi 
            
    Na Minael Msuya na Benjamin Mwangoka, Mwananchi 
            (email the author)
    
Posted Ijumaa,Julai12 2013 saa 10:41 AM
Posted Ijumaa,Julai12 2013 saa 10:41 AM
Kwa ufupi
 
Alisema, biashara ya dawa za kulevya 
inayoendelea  inatokana na tatizo la utoaji na upokeaji wa rushwa ambao 
unaongozwa na watu wakubwa, walioko katika mfumo halisi wa rushwa.
Dar es Salaam. Mwenyekiti wa 
Makampuni ya IPP, Reginald Mengi amesema, biashara ya dawa za kulevya 
inashamiri kutokana na tatizo la rushwa nchini.
Mengi alibainisha hayo jana katika uzinduzi wa  
ripoti ya mazingira ya ufanyaji wa biashara nchini 2013, iliyoandaliwa 
na Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF).
 Alisema, biashara ya dawa za kulevya 
inayoendelea  inatokana na tatizo la utoaji na upokeaji wa rushwa ambao 
unaongozwa na watu wakubwa, walioko katika mfumo halisi wa rushwa.
“Huwezi kutenganisha rushwa kubwa na dawa za 
kulevya, hawa wasichana wasanii wetu, waliokamatwa Afrika Kusini na dawa
 za kulevya na kile kiasi, lazima kuna mtu mkubwa aliye nyuma yao,siyo 
wao,” alisema Mengi.
  Mengi alisema,utashi wa Serikali katika 
kupambana na rushwa uko kisiasa ndiyo sababu hakuna utekelezaji na 
ikiendelea kuwakumbatia na kuwashikilia mkono watu hao nchi itadondoka.
    Alisema, taifa linatakiwa kuwatenga watoa 
rushwa na rushwa zao ili kuweza kuwa na taifa lenye nguvu kwa kuwa 
Serikali imeshindwa kupambana dhidi ya rushwa. kwa kuwa inahofia 
kukumbwa katika mfumo huo.
 Naye Mkurugenzi Mtendaji wa taasisi hiyo nchini, 
Godfrey Simbeye alisema mazingira ya kufanyia biashara nchini ni magumu 
kutokana na kodi nyingi na sheria ngumu zilizowekwa.
Simbeye alisema, utafiti unaonyesha kuwa suala la 
utozaji wa kodi limekuwa changamoto kubwa katika biashara kutokana na 
kuwa na kodi nyingi zisizoeleweka.
“Vikwazo vikubwa vinavyoyakabili mazingira ya 
ufanyaji wa biashara nchini ni kodi,  kumekuwa  na  kodi nyingi 
zinazotozwa na zisizoeleweka na sheria zilizowekwa zinaifanya biashara 
kuwa ngumu,” alisema.
 
  